Tuesday, April 17, 2012

MIAKA HAMSINI YA UHURU WA TANZANIA BARA

1
TAARIFA YA WIZARA YA
MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA
KIMATAIFA KWA KIPINDI CHA
MIAKA 50 YA UHURU WA
TANZANIA BARA
2
DIBAJI
1. Imewahi kuelezwa na mwandishi wa Kiingereza, Virginia
Woolf (1941) kuwa hakuna kitu kinaweza kusemwa kimetendeka hadi
kumbukumbu zake ziwe zimehifadhiwa. Ni dhahiri kuwa uandishi wa
kumbukumbu za yaliyotokea katika historia ya miaka 50 ya Uhuru wa
Tanzania Bara unaongozwa na busara hiyo. Na kwa kufanya
hivyo,tunafanya kitu chema kwa jamii ya Watanzania, hususan vizazi
vijavyo. Kumbukumbu hizi zitawaongoza kujenga Taifa lenye
maendeleo kuzidi yale yaliyokwishapatikana.
2. Kwa wanaokumbuka historia ya nchi yetu na ambayo
imedokezwa katika taarifa hii, hali ya uongozi wa kuthubutu
iliyojengeka tangu enzi ya kudai uhuru na miongo takriban mitatu
baadaye wakati wa utawala wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere, ndiyo iliyoifikisha nchi hii katika medani ya
kimataifa iliyotukuka. Mchango wa Mwalimu Nyerere katika kutetea
uhuru, haki na usawa wa wanyonge duniani unatambulika miongoni
mwa jamii ya kimataifa na imeelezwa katika taarifa hii kwa mifano.
3. Ni ukweli usiofichika kuwa uzoefu huleta majaribu mwanzoni
na baadaye mafunzo. Uzoefu wa nchi yetu kuzungukwa na mahasimu
wengi walioendeleza tawala za kikoloni na sera za ubaguzi wa rangi
3
mara baada ya uhuru wa nchi yetu, ulileta hofu mwanzoni lakini
taratibu tulipata kujifunza namna bora ya kukabiliana na hali hiyo.
Uzoefu huo ndiyo uliotufikisha hapa tulipo na ndiyo utatuongoza
tuendako miaka mingine 50 ijayo.
4. Taarifa hii ni ndefu si kwa makosa bali kwa kukusudia. Ni
dhahiri kuwa historia ya miaka 50 ya uhuru wa Tanzania Bara ni
pana. Kwa mantiki hiyo, historia ya Wizara hii ni pana kwani
inaelezea ilivyoanzishwa, muundo wake kadri ulivyokuwa
unabadilika, sera, majukumu na malengo yalivyokuwa yakipanuka
sanjari na hali ya uongozi na utawala, mabadiliko na matukio makuu
yaliyotokea, mafanikio yaliyopatikana hadi sasa, changamoto
zilizojitokeza na zinazoendelea kujitokeza na mwisho ni nini
matarajio ya wizara katika kipindi kingine cha miaka 50 ijayo. Yote
haya yameelezewa kwa kina katika taarifa hii ikiwa ni pamoja na
takwimu.
5. Ni matumaini yangu kwamba taarifa hii itasaidia sana
kuitambulisha Wizara kwenu nyinyi wadau na pia itasaidia watendaji
wa Wizara kujua wapi tumetoka na wapi tunakwenda. Kwa upande
wa watendaji, nawasihi kuwa kuisoma taarifa hii ni sehemu ya wajibu
wenu, lakini pia kuisoma na kuielewa haitoshi kama uelewa wenu
4
hautafuatiwa na utekelezaji wa yale ambayo hayakutekelezwa vema
siku za nyuma na kuboresha zaidi yale yaliyotekelezwa. Changamoto
za Wizara ni kubwa na nyingi lakini natarajia kuwa kwa pamoja
tunaweza kuzikabili.
6. Mwisho, natoa wito kwa Uongozi wa Wizara kuhakikisha
unasimamia majukumu tuliyopewa kwa mujibu wa Katiba ya Nchi,
Sheria, Kanuni, Taratibu na Amri Halali. Nawaomba muwe mstari wa
mbele kabisa katika kusimamia, bila woga, utekelezaji wa sera na
majukumu hayo na kuwa mfano bora wa kuigwa. Nina shauku kubwa
ya kuona Wizara inafanya vyema zaidi katika kipindi kijacho cha
miaka 50 kama Kauli mbiu ya Wizara inavyosema”UTENDAJI
BORA KULIKO JANA, NA BORA ZAIDI, KESHO”.
Bernard Kamillius Membe (Mb.)
WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA
USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
Juni, 2011
5
1.0 UTANGULIZI
Tanzania Bara imeanza kusherehekea miaka 50 ya uhuru wake. Huu
ni wakati muafaka wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa kuungana na Wizara, Idara zinazojitegemea, Mikoa na Wilaya
kueleza mafanikio ya kujivunia ambayo Nchi na Wizara imepata katika
medani ya mambo ya nje bila kusahau changamoto ambazo zinatukabili.
Taarifa hii inaanza kueleza, kwa ufupi kabisa, historia ya Wizara na Uongozi
na Utawala wake ulivyokuwa ukibadilika kukidhi utekelezaji wa sera,
majukumu na malengo ya Wizara na taifa kwa ujumla. Wakati wa kufanya
hayo, taarifa inabainisha mabadiliko na matukio makuu katika mfumo wa
kisiasa, kiulinzi, kiutawala, kiuchumi, kiteknolojia na kijamii. Vile vile,
taarifa inaeleza mafaniko na changamoto zilizoikabili na zinazoendelea
kuikabili Wizara na kumalizia kwa kudokeza juu ya mambo ambayo nchi na
Wizara inatarajia kufanya siku za usoni, kipindi cha kati hadi 2025 na baada
ya hapo.
2.0 HISTORIA FUPI YA WIZARA
2.1 Historia ya Wizara ya Mambo ya Nje, kama ilivyo kwa Wizara zote,
inaanzia pale Tanzania Bara (wakati huo Tanganyika) ilipopata uhuru
kutoka kwa Uingereza na hivyo hatuna budi kudokeza ukoloni ulivyoanza
na ulivyomalizika. Kama itakavyokumbukwa, Mkutano wa Berlin wa
Mataifa ya Ulaya wa kuligawa Bara la Afrika ulifanyika mwaka 1884 -
1885. Baada ya mkutano huo, Tanganyika iliwekwa chini ya utawala wa
Ujerumani. Kufuatia kumalizika kwa Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia (1914 -
1918), Tanganyika iliwekwa chini ya Shirikisho la Mataifa (League of
Nations) ikisimamiwa na Serikali ya Uingereza.
6
2.2 Ilipofika mwaka 1945 Umoja wa Mataifa ulianzishwa na mwaka
mmoja baadaye Tanganyika ikawekwa chini ya udhamini wa Umoja huo
huku ikiendelea kusimamiwa na Serikali ya Uingereza. Kuanzia wakati huo,
vuguvugu la kudai uhuru lililochochewa na wazalendo walioshiriki katika
Vita Kuu ya Kwanza na ya Pili ya Dunia liliongezeka kwa kasi kubwa zaidi.
Hali kadhalika, hamasa ya kuanzisha vyama vya siasa ilipamba moto. Moja
ya vyama hivyo ni chama cha Tanganyika African National Union (TANU)
kilichoanzishwa tarehe 7/7/1954. Hali hiyo ndiyo iliyosababisha kuitishwa
kwa uchaguzi mkuu wa mwaka 1960 ambapo TANU ilipata idadi kubwa ya
viti vya Ubunge.
2.3 Ushindi huo ulitoa nafasi kwa chama hicho kuunda Serikali ya
Madaraka ya Ndani mnamo mwezi Mei, 1961 na Mwenyekiti wa TANU,
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akawa Waziri Mkuu Mteule. Miezi
saba baadaye, Tanganyika ikapata uhuru wake kutoka utawala wa
Mwingereza tarehe 9 Disemba, 1961 na Mhe. Julius Kambarage Nyerere
akawa Waziri Mkuu wa kwanza. Makabidhiano ya madaraka na alama za
Taifa yalifanyika saa sita za usiku wa tarehe 8 kuamkia tarehe 9 Disemba,
1961 ambapo bendera ya Uingereza ilishushwa na ya Tanganyika
kupandishwa ikiwa ni ishara ya kuisha kwa utawala wa Mwingereza chini ya
Gavana wake wa mwisho, Sir Richard Turnbull.
2.4 Kuanzia hapo, masuala ya mambo ya nje yakawa chini ya Waziri
Mkuu yakiratibiwa na Idara ya Mambo ya Nje na Ulinzi. Alipojiuzulu nafasi
ya Waziri Mkuu tarehe 22 Januari, 1962 masuala hayo yaliendelea kuwa
chini ya Waziri Mkuu aliyefuata, Mheshimiwa Rashid Mfaume Kawawa.
Tarehe 14 Disemba, 1961 Tanganyika ilijiunga rasmi na Umoja wa Mataifa.
7
Ilipofika tarehe 9 Disemba, 1962 Tanganyika ikawa Jamhuri na Mwalimu
Julius Kambarage Nyerere akawa Rais wa kwanza na Jamhuri ikajiunga na
Jumuiya ya Madola.
2.5 Kutokana na umuhimu wa kukabiliana na masuala ya yaliyokuwepo
wakati huo, Serikali iliimarisha Idara ambayo baadaye ilikuja kuwa Wizara.
Aidha, kwa vile Tanzania haikuwa na balozi nje na kulikuwa na majukumua
ya kutekeleza, Serikali iliteua watendaji wa Idara na wawakilishi nje,
ikatafuta ofisi, nyumba za kuishi na vitendea kazi muhimu. Mhe. Dkt.
Vedast Kyaruzi aliteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa kwanza wa Idara ya
Mambo ya Nje na Ulinzi ambaye alishikilia Idara hiyo hadi mwaka 1962
mwishoni. Mnamo Disemba, 1962 Serikali iliteua Mabalozi wake katika
kituo cha London, Uingereza na Ofisi ya Kudumu ya Umoja wa Mataifa
huko New York, Marekani. Mabalozi hao walikuwa ni Mhe. Dustan Omari
kuwa Balozi wa Tanzania nchini Uingereza na Mhe. Dkt. Vedast Kyaruzi
ambaye alihamishiwa Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, New
York. Aidha, Serikali ilifungua milango kwa nchi za nje kufungua Ofisi zao
za uwakilishi hapa nchini. Serikali za Uingereza na Ujerumani zilikuwa ni
nchi za kwanza kufungua Balozi zao hapa nchini.
2.6 Kuanzia uhuru hadi sasa, Wizara imetekeleza kwa mafanikio ya
kujivunia sera yake ya mambo ya nje: kutetea haki za wanyonge na nchi
maskini; kupiga vita ukoloni; ukoloni mamboleo, na siasa za ubaguzi;
kuendeleza umoja wa Afrika; na, kuunga mkono sera ya kutofungamana na
upande wowote. Masuala haya yalibainishwa baadaye kupitia Waraka wa
Rais Na. 2 wa mwaka 1964 uliotolewa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere. Kwani, Waraka huo ndio ulioainisha waziwazi sera,
muundo na majukumu ya Wizara. Mafanikio ya utekelezaji wa sera hiyo ni
8
pamoja na mchango mkubwa wa Wizara na nchi katika kulinda uhuru wetu,
kutetea haki za wanyonge, ukombozi wa nchi za kusini mwa Afrika,
kutokomeza siasa za ubaguzi wa rangi Afrika Kusini, pamoja na kujenga
umoja na mtangamano wa kikanda na Bara la Afrika.
2.7 Sera hiyo ilidumu hadi miaka ya 1990 ambapo majukumu haya
yalipanuliwa kufuatia kukamilika kwa mchakato wa ukombozi, ikiwa ni
pamoja na kukomeshwa kwa siasa za kibaguzi nchini Afrika Kusini,
kumalizika kwa vita baridi, kuibuka kwa utandawazi na mageuzi ya kisiasa,
kiuchumi na kijamii hususan, mfumo wa vyama vingi vya siasa.
2.8 Baada ya kupata mafanikio katika maeneo hayo, sera ya mambo ya
nje iliweka mkazo pia katika masuala ya kukuza uwekezaji, biashara na
utalii ili kuchochea maendeleo ya nchi ikimaanisha kwamba majukumu yake
yakawa yameongezeka kama yanavyofafanuliwa katika sehemu ya nne ya
Taarifa hii.
3.0 MUUNDO WA WIZARA
3.1 Baada ya Tanzania Bara kupata uhuru wake na baadaye kuwa
Jamhuri, muundo wa Wizara ulikuwa ni Idara ya Mambo ya Nje na Ulinzi
iliyokuwa ikisimamiwa na Waziri Mkuu. Idara hiyo ilikuwa na Divisheni ya
Mambo ya Nje na ya Ulinzi. Mnamo Disemba, 1963 Idara ya Mambo ya Nje
na Ulinzi ilibadilishwa na kuwa Wizara ya Mambo ya Nje na Ulinzi. Mhe
Oscar Kambona aliteuliwa kuongoza Wizara hiyo.
3.2 Tarehe 26 Aprili, 1964 Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu
wa Zanzibar ziliungana na kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na
9
Zanzibar na baadaye nchi hii iliyotokana na muungano huo ikaitwa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania. Kutokana na tukio hilo la kihistoria, Wizara ya
Mambo ya Nje ikawa moja ya Wizara za Muungano. Kwa ajili hiyo,
ikajulikana kama Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na ikachukua sura ya muungano na kuwa chini ya Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania.
3.3 Mwaka 1965, Wizara ya Mambo ya Nje ilitenganishwa na Ulinzi
lakini iliendelea kuwa chini ya Ofisi ya Rais akisaidiwa na Waziri wa Nchi
mwenye dhamana ya Mambo ya Nje. Muundo huo uliendelea hadi Januari,
1972 ambapo Mhe. Balozi Mstaafu John S. Malecela aliteuliwa kuwa
Waziri wa Mambo ya Nje.
3.4 Ilipofika mwaka 1987, jina la Wizara lilibadilika na kuwa Wizara ya
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa baada ya kuongezewa
majukumu ya kuratibu masuala ya ushirikiano wa kikanda na kimataifa.
Kufuatia mabadiliko hayo, Wizara iliongozwa na Waziri akisaidiwa na
Waziri wa Nchi aliyepewa dhamana ya kushughulikia masuala ya
ushirikiano wa kikanda na kimataifa. Kiutendaji, Wizara iliendelea
kuongozwa na Katibu Mkuu akisaidiwa, kwa mara ya kwanza, na Naibu
Katibu Mkuu.
3.5 Kuanzia mwaka 2005, Wizara ikawa inaongozwa na Waziri,
akisaidiwa na Naibu Waziri wawili. Naibu Waziri mmoja alishughulikia
masuala ya siasa na mwingine ya uchumi. Katibu Mkuu aliendelea
kusaidiwa na Naibu Katibu Mkuu.
10
3.6 Kufuatia mabadiliko ya Baraza la Mawaziri ya mwaka 2008, Wizara
ikabaki chini ya uongozi wa Waziri, Naibu Waziri mmoja, Katibu Mkuu na
Naibu Katibu Mkuu, hadi sasa.
3.7 Kwa maelezo hayo, muundo wa Wizara umekuwa ukibadilika
kulingana na majukumu yalivyokuwa yakiongezeka kwa kuzingatia
mahusiano kati ya nchi na nchi pamoja na mashirika ya kimataifa,
utandawazi, maendeleo ya sayansi na teknolojia, biashara na utangamano
kupitia jumuiya na taasisi mbalimbali za kikanda na kimataifa.
3.8 Muundo unaotumika mpaka wakati wa taarifa hii ni ule uliopitishwa
tarehe 9/10/2010 baada ya kuongezeka Idara ya Diaspora na hivyo kuifanya
Wizara kuwa na Waziri na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu
Mkuu, na Idara 11; Vitengo sita; Balozi 32 na Balozi Ndogo tatu. Aidha,
Wizara inasimamia taasisi mbili ambazo ni Kituo cha Mikutano cha
Kimataifa cha Arusha (AICC), na Chuo cha Diplomasia (CFR) kilichopo
Dar es Salaam. Maelezo ya Taasisi hizo yamo pia katika taarifa hii.
3.9 Orodha za Mawaziri na Makatibu Wakuu waliowahi kuongoza
Wizara tangu na baada ya uhuru hadi sasa inaonekana katika Jedwali Na. I
na Jedwali Na. II hapa chini:
Jedwali Na. I (Mawaziri)
Na. Jina Kipindi
Toka
Hadi
1. Waziri Mkuu Mwenyewe 9/12/1961 1963
2. Mhe. Oscar Kambona 1963 1966
3. Mhe. Chediel Mgonja 1967 1969
4. Mhe. Stephen Mhando 1969 1970
5. Mhe. Israel Elinawinga 1971 1972
11
Chanzo: Wizara ya Mambo ya Nje na Idara ya Nyaraka za Serikali
Jedwali Na. II (Makatibu Wakuu)
Na. Jina Kipindi Toka Hadi
1. Bw. Co. W. B. Rogers 01.05.1961 24.09.1961
2. Dkt. Vedast K. Kyaruzi 18.03.1962 30.09.1963
3. Bw. Amon Nsekela 01.10.1963 17.02.1964
4. Chifu Mwinamila M.J.S.
Lukumbuzya
18.02.964 04.10.1965
5. Bw. Bernard Mulokozi 05.10.1965 19.01.1968
6. Bw. Obed M. Katikaza 20.01.1968 04.11.1970
7. Bw. Daniel N. M. Mloka 05.11.1970 17.02.1972
8. Bw. Anthony B. Nyakyi 18.02.1972 26.12.1978
9. Bw. Daniel N. M. Mloka 27.12.1978 28.08.1981
10. Bw. Gilman Rutihinda 29.08.1981 23.04.1984
11. Bw. Paul Rupia 24.04.1984 27.06.1986
12. Bw. Ashour A. Abbas 28.06.1986 13.11.1990
13. Bw. Crispian Mbapila 14.11.1990 09.12.1992
14. Dkt. Ibrahim Msabaha 10.12.1992 30.08.1995
15. Bw. Abdi H. Mshangama 31.8.1995 19.12.1995
16. Bw. Elly E. Mtango 19.12.1995 13.02.2000
17. Bw. Hassan O. G. Kibelloh 14.02.2000 21.01.2002
6. Mhe. John S. Malecela 1972 1974
7. Mhe. Ibrahim Kaduma 1975 1976
8. Mhe. Benjamin W. Mkapa 1977 1980
9. Mhe. Salim A. Salim 1981 1984
10. Mhe. Benjamin W. Mkapa 1984 1990
11. Mhe. Hassan Diria 1991 1992
12. Mhe. Joseph Rwegasira 1993 1995
13. Mhe. Jakaya M. Kikwete 1995 2005
14. Mhe. Dkt. Asha-Rose Migiro 2005 2007
15. Mhe. Bernard K. Membe 2007 Hadi sasa
12
18. Bw. Phillemon L. Luhanjo 19.07.2002 21.01.2006
19. Bw. Charles Mutalemwa 21.01.2006 28.11.2006
20. Bw. Patrick Mombo 29.11.2006 31.12.2008
21. *Bw. Seth Kamuhanda 01.01.2009 18.10.2009
22. Bw. Sazi B. Salula 19.10.2009 28.02.2011
23. Bw. John M. Haule 01.03.2011 Hadi sasa
Chanzo: Sekretariati ya Baraza la Mawaziri. Bw. Seth Kamuhanda ameingizwa
katika jedwali hili kwa sababu alikuwa Naibu Katibu Mkuu aliyekaimu shughuli za
Katibu Mkuu kwa kipindi hicho.
4.0 MAJUKUMU NA MALENGO YA WIZARA
4.1 Tangu Tanzania Bara ipate uhuru wake, Wizara imekuwa na
majukumu makuu au ya msingi tisa (9) yaliyoainishwa katika hati dhamana
kama ifuatavyo: kubuni na kusimamia utekelezaji wa sera ya mambo ya nje;
kusimamia mikataba na makubaliano ya kimataifa; kuratibu masuala ya
ushirikiano ya kimataifa, kikanda na Bara la Afrika; kulinda na kuendeleza
maslahi ya kitaifa ya kiuchumi na mengineyo huko nje; kusimamia masuala
yanayohusu kinga na upendeleo maalum kwa wanabalozi walioko nchini;
kusimamia na kuratibu masuala ya itifaki na uwakilishi; kuanzisha na
kusimamia huduma za kikonseli; kuratibu shughuli za Tume za Pamoja za
Kudumu za ushirikiano; na utawala na maendeleo ya utumishi Wizarani na
kwenye Balozi zetu Nje. Majukumu hayo yametokana na sera ya nje
iliyoelezwa hapo juu.
4.1.1 Katika miaka ya sitini hadi themanini, Wizara ilijishughulisha sana
na suala la ulinzi wa uhuru na mipaka ya nchi yetu. Kama ilivyokuwa
kwa utekelezaji wa masuala mengine, Wizara ilifanya hivyo kwa
kutumia njia nyingi ikiwemo kupitia ushawishi mkubwa na misimamo
thabiti katika taasisi za kikanda na za kimataifa. Taasisi hizo ni
13
pamoja na: Nchi za Mstari wa Mbele (Front Line States) na Klabu ya
Mulungushi kabla yake, Umoja wa Nchi huru za Kiafrika (OAU),
Umoja wa Wakereketwa wa Uhuru na Utu wa Mwafrika na Watu
Weusi (Pan-African Movement), nchi zisizofungamana na upande
wowote, Jumuiya ya Madola na Umoja wa Mataifa. Wakati wote
Tanzania ilifanya jitihada kubwa ili kupata sauti ya pamoja katika
masuala yote yaliyohusu maslahi ya nchi na Afrika. Vile vile jitihada
hizo zilifanywa katika kuhakikisha amani na usalama na haki katika
Jumuiya yote ya Kimataifa vinapatikana.
4.1.2 Mara baada ya uhuru msimamo wa Tanzania juu ya mipaka ulikuwa
ni kutaka mikataba ya kikoloni kuhusu mipaka iangaliwe upya ili
kuondoa vipengele ambavyo vilikuwa havikidhi maslahi halisi ya
Tanzania na nchi za Afrika kwa jumla. Kuhusu Tanzania, barua
ilipelekwa Umoja wa Mataifa ikieleza kwamba Serikali ingelifanyia
mapitio mikataba hiyo badala ya kuirithi kama ilivyokuwa na kazi
hiyo ilifanyika. Kuhusu Afrika suala hilo lilitolewa msimamo na
Azimio la OAU la Cairo la 1964 kuhusu mipaka. Sera hiyo
imeiongoza Tanzania wakati wote ambapo nchi moja ya kiafrika
iliingilia uhuru na mipaka ya nchi nyingine au wakati majeshi ya
kukodishwa yalipotumika kufanya mapinduzi katika nchi za kiafrika.
4.1.3 Tanzania ilipovamiwa na Nduli Iddi Amin wa Uganda mwaka 1978,
jitihada za kutosha zilifanyika kubainisha kwamba kitendo hicho
kilikuwa cha uvamizi na kilikuwa kinakiuka msingi wa Umoja wa
Afrika wa kuheshimu uhuru wa nchi na mipaka yake na kuzitaka nchi
wanachama wa OAU zilaani kitendo hicho. Jitihada za kutosha
zilifanyika vilevile kueleza Jumuiya ya Kimataifa kwamba kitendo
14
hicho kilikuwa kimevunja Katiba ya Umoja wa Mataifa na kuwaomba
waelewe uhalali wa hatua ambazo Tanzania ilikuwa imechukua dhidi
ya uvamizi huo.
4.2 Kwa kuzingatia kwamba Tanzania haikuwa huru na salama katika
mipaka yake hadi nchi zote za Afrika zipate uhuru wake, Tanzania
ilichangia sana katika harakati za ukombozi, hususan wa nchi zilizo kusini
mwa Afrika ikiwa ni pamoja na Msumbiji, Angola, Namibia, Zimbabwe na
Afrika Kusini. Ilijishughulisha pia na ukombozi wa visiwa vya Comoro,
Shelisheli na Sao-Tome & Principe, Guinea Bissau na Western Sahara.
Tanzania ilijihusisha pia na masuala ya ukombozi nje ya Afrika kama vile
kule Palestine.
4.2.1 Katika harakati hizo, nchi yetu ilijitolea mhanga kwa kutoa misaada
ya hali na mali ili kupambana na udhalimu wa ukoloni kwa
kushirikiana na nchi nyingine pamoja na wapigania uhuru wa nchi
hizo. Aidha, Vyama vya Ukombozi vya nchi hizo vilipewa hifadhi
katika nchi yetu, na kupatiwa mafunzo kwa wanachama wao ikiwa ni
pamoja na kuwaruhusu wapokee vifaa vyao kupitia Tanzania na
kuvisafirisha kuelekea nchini mwao. Vyama vya ukombozi
vilivyonufaika zaidi na mchango wa Tanzania ni pamoja na
FRELIMO cha Msumbiji, MPLA na UNITA vya Angola, SWAPO
cha Namibia, ZANU na ZAPU vya Zimbabwe na ANC na PAC vya
Afrika Kusini. Urafiki uliojengeka tangu wakati huo kati ya Vyama
hivyo na TANU na Afro-Shirazi na baadaye na CCM unaendelea hadi
sasa.
15
4.2.2 Ikumbukwe kwamba, Tanzania Bara, ukiondoa DRC, ilikuwa nchi ya
kwanza kupata uhuru katika nchi zote za Afrika ya Mashariki, Kati na
Kusini mwa Afrika. Nchi yetu ilikuwa imezungukwa na nchi ambazo
zilikuwa bado zinatawaliwa na wakoloni zikiwemo: Zanzibar, Kenya,
Uganda, Zambia, Malawi na Shelisheli zilizokuwa zinatawaliwa na
Mwingereza; Msumbiji iliyokuwa inatawaliwa na Ureno pamoja na
Rwanda na Burundi zilizokuwa zinatawaliwa na Ubelgiji. Wakati huo
huo Zaire (sasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo) ambayo ilipata
uhuru wake kutoka kwa Ubelgiji mwaka 1960, ilikuwa katika
machafuko ya kisiasa. Kwa kuzingatia kwamba uhuru na usalama wa
Tanzania ulikuwa hatarini, Tanzania haikuwa na budi kusaidia nchi
zote kujikomboa.
4.2.3 Kwa kutambua mazingira hayo na mchango wa Tanzania, Umoja wa
Nchi Huru za Afrika uliamua kuwa Tanzania iwe mwenyeji wa
Kamati yake ya Ukombozi. Hivyo, Kamati hiyo iliundwa mwaka
1963 na kuwa na Makao Makuu yake jijini Dar es Salaam. Wizara ya
Mambo ya Nje ilikuwa na jukumu la kuratibu shughuli za Kamati
hiyo kupitia Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU). Aidha, kati ya
mwaka 1972 na 1980 Mhe. Dkt. Salim Ahmed Salim, akiwa
Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania kwenye Umoja wa Mataifa
alikuwa Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Umoja wa Mataifa
iliyoshughulikia uhuru wa nchi za Afrika - The United Nations
Special Committee on Decolonization – Committee of 24. Kamati
hiyo ilifanya kazi kubwa sana ya kujenga muafaka wa hatua
zilizopaswa kuchukuliwa na jumuiya ya kimataifa ili kuharakisha
uhuru kupatikana kwenye nchi ambazo zinatawaliwa na kusaidia
16
kupatikana uhuru kamili katika nchi mbalimbali hasa za kusini mwa
Afrika.
4.2.4 Tanzania ilikuwa mwanachama asiye wa kudumu wa Baraza la
Usalama wa Umoja wa Mataifa mwaka 1975 hadi 1976, na ikatumia
nafasi hiyo adimu kushawishi kwa bidii kubwa zaidi mataifa
makubwa na Jumuiya ya Kimataifa kwa jumla juu ya umuhimu wa
kuzipatia uhuru nchi za Afrika zilizokuwa zikiendelea kukaliwa
kimabavu na wakoloni. Kutokana na jitihada hizo za ziada nchi ya
Msumbiji na baadaye nchi za Angola na Visiwa vya Cape Verde &
Principe zilipata uhuru wao mara baada ya Serikali ya Ureno
kupinduliwa.
4.2.5 Aidha, matokeo ya jitihada hizo yalipelekea pia kuanguka kwa
utawala wa kidhalimu wa Ian Smith wa Zimbabwe mnamo mwaka
1980 na baadaye utawala dhalimu na wa ubaguzi wa rangi wa Afrika
Kusini mnamo mwaka 1990 ambazo zilikuwa ni vyanzo vya uhasama
baina ya nchi yetu na baadhi ya nchi za nje ikiwa ni pamoja na
majirani zetu.
4.3 Wizara imeratibu kwa mafanikio makubwa ushiriki wa Tanzania
katika mchakato wa uanzishaji wa Umoja wa Afrika na masuala yote yenye
maslahi kwa Afrika kuanzia miaka ya sitini hadi sasa. Kuanzishwa kwa
umoja huu kulichochea harakati za ukombozi kama ilivyoelezwa hapo juu.
Kutokana na mchango wake, Tanzania ikawa mwenyeji wa Kamati ya
Ukombozi ya OAU.
17
4.3.1 Aidha, kati ya mwaka 1971 na 1982 Tanzania, chini ya uenyekiti wa
Mhe. Jaji Mstaafu Joseph S. Warioba, Waziri Mkuu Mstaafu, pamoja
na nchi wanachama wengine wa OAU walishiriki kikamilifu katika
majadiliano yaliyopelekea kupitishwa kwa Mkataba wa Kimataifa wa
Sheria ya Bahari. Mkataba huu ulikuwa na manufaa kwa nchi
wanachama kwani uliwezesha kusimamia matumizi ya bahari na
rasilimali zake kwa usawa hivyo kuzuia migongano.
4.3.2 Mchango mkubwa wa Tanzania katika mafanikio haya umeiletea nchi
yetu sifa na heshima kubwa katika bara la Afrika na jumuiya ya
kimataifa kwa ujumla na kuimarisha uhusiano na nchi hizi na hivyo
kujenga msingi imara wa kukuza ushirikiano katika nyanja za
biashara, uwekezaji na maeneo mengine ya kijamii.
4.3.3 Tanzania imejijengea pia heshima kubwa ndani ya OAU kwa kutoa
uongozi wa juu. Mbali ya Jaji Warioba kuongoza majadiliano ya
Mkataba wa Kimataifa wa Sheria ya Bahari, Mhe. Salim A. Salim,
Waziri Mkuu Mstaafu, aliongoza umoja huo kama Katibu Mkuu kwa
vipindi viwili mfululizo na kuuletea maboresho makubwa likiwemo
mchakato wa kugeuza OAU kuwa Umoja wa Afrika (AU). Vile vile
Mhe. Balozi Mstaafu Getrude I. Mongela alichaguliwa kuwa Spika
wa kwanza wa Bunge la Umoja wa Afrika tarehe 19 Machi, 2004.
4.3.4 Aidha, katika ngazi ya Uenyekiti, Tanzania ilipata nafasi ya kuwa
Mwenyekiti mara mbili ambapo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius K.
Nyerere, alishika nafasi hiyo mwaka 1984 – 1985 na Mhe. Jakaya M.
Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliongoza
umoja huo kama Mwenyekiti mwaka 2008 ambapo pamoja na mambo
18
mengine, aliboresha maslahi ya wafanyakazi wa Sekretarieti ya
Umoja huo.
4.3.5 Mjadala wa kuundwa kwa Serikali moja ya Afrika ambao ulianza hata
kabla ya kuundwa kwa OAU bado unaendelea. Tanzania siku zote
imeshikilia kwamba njia pekee ya kufikia muungano kamili wa Afrika
yenye Serikali moja ni ya hatua moja baada ya nyingine na kwamba
fikra za kwamba Serikali ya Afrika inaweza kuanzishwa kwa hatua
moja haitekelezeki. Katika kuonyesha mfano wa kujenga Umoja huo,
Jamhuri ya Tanganyika iliungana na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar
tarehe 26 Aprili, 1964 na kuunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Msimamo wa Tanzania kuhusu kufikia Serikali moja ya Afrika ni
pamoja na kwanza kuimarisha jumuiya za kiuchumi za kikanda
ambazo baadaye zitaungana na kufanya jumuiya moja barani Afrika
na hatimaye Serikali moja.
4.4 Kwa kutambua umuhimu katika uhusiano wa kila siku na wa kudumu
miongoni mwa mataifa, Wizara imekuwa na jukumu la kusimamia,
kuanzisha na kuimarisha ujirani mwema. Kwa mfano, Tanzania ilishiriki
katika mapambano dhidi ya ukoloni na ubaguzi wa rangi kupitia vikundi
mbalimbali hususan Klabu ya Mulungushi iliyoundwa na nchi za Tanzania,
Zambia, na Uganda kabla ya Serikali ya Milton Obote kupinduliwa mwaka
1971.
4.4.1 Klabu ya Mulungushi ilifuatiwa na Nchi za Mstari wa Mbele (Front
Line States – FLS) ambazo zilikuwa ni: Tanzania, Zambia, Botswana,
Nigeria na vyama vya Ukombozi vya ANC, ZANU, ZAPU na
SWAPO. Angola, Msumbiji, Zimbabwe na Namibia zilijiunga baada
19
ya kupata uhuru. Jukumu hili limefanikiwa kutokana na historia ya
nchi yetu, urafiki wa watu wetu na pia kufanyika kwa vikao vya
ujirani mwema baina ya nchi yetu na nchi za jirani. Aidha, mikutano
ya Tume za Pamoja za Kudumu za Ushirikiano na ziara za viongozi
za kitaifa zimekuwa chachu ya kuendeleza uhusiano na ushirikiano
wa ujirani mwema.
4.4.2 Hata hivyo, uhusiano wetu na baadhi ya nchi jirani na nyinginezo
haukuwa mzuri siku zote. Kwa mfano, mzozo baina yetu na Malawi
kuhusu mpaka katika Ziwa Nyasa uliendelea na kukuzwa kwa sababu
ya urafiki wa Serikali ya Malawi na Afrika Kusini. Aidha, Tanzania
ilinuniwa na baadhi ya mataifa makubwa baada ya kutoa mchango
mkubwa katika Baraza la Kuu la Umoja wa Mataifa ulioiwezesha
Jamhuri ya Watu wa China kupata uanachama wa Umoja wa Mataifa.
Kadhalika, uhusiano wa Tanzania na Kenya ulidorora na hata
kupelekea kufungwa kwa mpaka baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya
Afrika Mashariki mwaka 1977. Vile vile uvamizi wa ardhi ya
Tanzania uliofanywa na majeshi ya Iddi Amin wa Uganda tarehe 4
Novemba, 1978 ulisababisha uhasama na hatimaye vita kati yetu na
majeshi yake iliyomalizika mnamo Julai 1979. Vita hiyo ilimng’oa
Iddi Amin ambaye hatimaye alikimbilia uhamishoni Saudi Arabia.
4.5 Wizara imekuwa ikiratibu na kushiriki kikamilifu katika kuendeleza
siasa ya kutofungamana na upande wowote kutokana na kuthamini uhuru wa
nchi kujiamulia mambo yake yenyewe. Kwa mfano, mwaka 1965 Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilivunja uhusiano wa kibalozi na
iliyokuwa Serikali ya Ujerumani Magharibi, wakati Serikali hiyo ilipotaka
20
kushurutisha Serikali yetu kutoitambua iliyokuwa Serikali ya Ujerumani
Mashariki.
4.6 Aidha, Tanzania imekuwa ikishiriki kikamilifu kwenye mikutano
mbalimbali ya kikanda na kimataifa inayotafuta msimamo wa pamoja
wa nchi masikini za dunia katika kulinda haki zao. Hali kadhalika,
Tanzania imekuwa ikishiriki kikamilifu katika shughuli za Umoja wa
Mataifa pamoja na mikutano ya Nchi Zisizofungamana na upande
wowote. Katika ushiriki huo, Tanzania imekuwa ikiweka bayana
msimamo wake wa kupigania usawa wa binadamu, kupiga vita
ukoloni na kutetea maendeleo ya nchi changa.
4.7 Baada ya nchi za kusini mwa Afrika kujikomboa, dunia iliingia katika
wimbi la mageuzi makubwa katika nyanja mbalimbali. Kati ya 1989 na 1990
ukuta wa Berlin uliokuwa unatenganisha Ujerumani Mashariki na
Ujerumani Magharibi ulibomolewa na kupelekea kuungana tena kwa nchi
hiyo. Aidha, katika kipindi hicho tawala nyingi za kikomunisti zilizokuwa
katika nchi za Ulaya ya Mashariki zilisambaratika. Pia mwaka 1991 Jamhuri
ya Kisoshalisti ya Urusi, nchi ambayo ilikuwa mhimili mkubwa wa kambi
ya Mashariki wakati wa vita baridi, ilisambaratika. Mabadiliko hayo
yakapelekea kumalizika kwa vita baridi na kuzuka kwa taifa moja lenye
nguvu.
4.8 Hali hiyo ikachochea mageuzi makubwa duniani ikiwa ni pamoja na:
kuimarika kwa soko huria na mitaji; kushamiri kwa uchumi huria na
utandawazi; mabadiliko kutoka misaada ya maendeleo hadi ushirikiano wa
kibiashara; kuibuka kwa vuguvugu la kuzingatia haki za binadamu, utawala
21
bora na demokrasia; na, kuzuka kwa changamoto za pamoja kama vile
ugaidi wa kimataifa, uharamia, biashara haramu ya watu na mihadarati.
4.9 Kwa kuzingatia mabadiliko hayo, Tanzania ilikuwa haina budi kubuni
sera mpya ambayo ingesaidia kuhakikisha kwamba misingi ya sera ya awali
inadumishwa na kwa wakati huo huo kuiwezesha nchi kukabiliana na
changamoto ambazo zilijitokeza duniani kote. Hivyo, mwaka 2001, Sera ya
Mambo ya Nje ilihuishwa ili kuzingatia changamoto hizo.
4.10 Misingi ya sera mpya ikawa ni kulinda uhuru wa kujiamulia mambo
yetu wenyewe; kuheshimu mipaka ya nchi na uhuru wa kisiasa; kulinda
uhuru, haki za binadamu, usawa na demokrasia; kukuza ujirani mwema;
kuendeleza Umoja wa Afrika; kukuza ushirikiano wa kiuchumi na wabia wa
maendeleo; kuunga mkono utekelezaji wa sera ya kutofungamana na upande
wowote na ushirikiano wa nchi maskini duniani; na kuunga mkono Umoja
wa Mataifa katika jitihada zake za kuimarisha maendeleo ya uchumi wa
kimataifa, amani na usalama. Hayo yote yametekelezwa kwa ukamilifu na
ufanisi mkubwa.
4.11 Kwa ujumla, ikiwa kama mratibu wa sera ya mambo ya nje, Wizara
inaendelea kutambua michango mbalimbali ya Wizara nyingine na taasisi
katika kuhakikisha kuwa misingi na malengo ya sera ya mambo ya nje
inasimamiwa na kutekelezwa. Hii inatokana na kwamba sera ya mambo ya
nje ni mtambuka na mwendelezo wa sera nyingine za ndani ya nchi katika
nyanja na maeneo mbalimbali ya kiuchumi na kijamii.
22
5.0 HALI YA UONGOZI NA UTAWALA KUANZIA 1961
5.1 Wakati tulipopata uhuru, Tanzania Bara ilikabiliwa na upungufu
mkubwa wa watumishi na viongozi waliokuwa na elimu na ujuzi wa
kutekeleza majukumu yaliyokuwepo. Upungufu huo ulijionyesha wazi
katika Idara ya Mambo ya Nje na Ulinzi. Tatizo hilo lilishughulikiwa kwa
Serikali kuajiri watumishi na viongozi kutoka nje hasa wale ambao
walikuwa wakitumikia Serikali ya Mwingereza.
5.2 Vile vile, katika kutatua tatizo hilo Serikali ililazimika kuhamisha
watumishi na viongozi kutoka Wizara na Idara nyingine ili kuziba mapengo
katika Idara ya Mambo ya Nje na Ulinzi. Hata hivyo, sehemu kubwa ya
watumishi na viongozi waliochukuliwa hawakuwa na shahada ya chuo kikuu
ambayo ndiyo moja ya sifa muhimu ya kujiunga na Idara kama Ofisa
Mambo ya Nje. Pamoja na mpango maalum uliokuwa wa kuwapa
wazalendo nafasi za kazi zilizokuwa zinashikiliwa na wageni
(Afrikanaizesheni), hali hiyo iliendelea mpaka miaka ya sabini na kuanzia
hapo Wizara ikawa haiajiri tena watumishi wasiokuwa na sifa hiyo.
5.3 Kutokana na unyeti usio na kifani wa Mambo ya Nje wakati ule
ulioletekezwa, pamoja na mambo mengine, kuzungukwa na majirani wote
waliokuwa bado wakitawaliwa na Uingereza, Ubelgiji na Ureno, Idara ya
Mambo ya Nje na Ulinzi ilikuwa chini ya Waziri Mkuu na baadaye chini ya
Rais. Waziri wa kwanza mwenye dhamana ya Mambo ya Nje na Ulinzi,
Mhe. Oscar Kambona, aliteuliwa mwaka 1963 na hivyo Idara ikawa na
Waziri pamoja na Katibu Mkuu. Wakati huo Zanzibar, Kenya, Uganda na
Zambia zilikuwa zimepata uhuru au ukingoni mwa kupata uhuru wao.
23
5.4 Kufuatia muungano baina ya Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964,
Waziri wa Mambo ya Nje aliendelea na dhamana hiyo ambayo ilichukua
sura ya muungano. Kuanzia wakati huo, masuala mbalimbali ya Wizara
ikiwa ni pamoja na uongozi, utumishi na uwakilishi nje ya nchi umekuwa
ukizingatia pande zote mbili za Muungano.
5.5 Ikumbukwe kwamba sifa za kuwezesha mtumishi wa umma kuajiriwa
katika Wizara hazikuishia katika uraia, kisomo na ujuzi au utaalam tu bali
pia ilikuwa muhimu mwajiriwa awe mwanachama wa Chama Tawala wakati
wote wa utawala wa chama kimoja. Aidha, ilikuwa muhimu pia mtumishi
awe amepitia mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa mujibu wa sheria kwa
Maafisa Mambo ya Nje au Mgambo kwa kada zingine. Sifa hizo ziliwezesha
Wizara na Serikali yote kwa jumla kuwa na watumishi na viongozi wenye
maadili mazuri na nidhamu kubwa.
5.6 Kadhalika, katika kudumisha uongozi na utawala bora, kumekuwa na
Baraza la Wafanyakazi imara katika Wizara kuanzia mwaka 1967 wakati
Azimio la Arusha lilipoanzishwa. Baraza linaendelea kukutana mara mbili
kila mwaka chini ya Uenyekiti wa Mhe. Waziri na limekuwa kiungo kizuri
kati ya menejimenti na wafanyakazi.
6.0 SERA NA SHERIA ZILIZOKUWEPO TANGU 1961 HADI SASA
6.1 Waraka wa Rais Na. 2 wa mwaka 1964 tulioueleza hapo juu, ndiyo
mwongozo wa kwanza uliobainisha misingi ya sera yetu ya Mambo ya Nje.
Kabla ya hapo, misingi hiyo ilikuwa inafuatwa bila kuwepo waraka. Misingi
iliyopo katika waraka huo iliendelea kuongoza Wizara hadi mwaka 2001
24
ambapo Wizara ilihuisha sera yake kwa kuzingatia mabadiliko yaliyokuwa
yametokea duniani.
6.2 Kwa upande wa utawala, Wizara imekuwa ikiongozwa na sheria,
kanuni na taratibu za utumishi wa umma ambazo husimamiwa na Idara Kuu
ya Utumishi pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu. Aidha, kwa upande wa fedha
na ununuzi, Wizara imekuwa ikiongozwa na sheria, kanuni na taratibu za
matumizi ya fedha za serikali zinazosimamiwa na Wizara ya Fedha. Sheria,
Kanuni na Taratibu hizo zimekuwa zikipitiwa na kuboreshwa pale inapobidi.
6.3 Aidha, kutokana na majukumu ya mambo ya nje, Wizara pia
inaongozwa na Kanuni za Utumishi wa Umma Nje ya Nchi (Foreign Service
Regulations) ambazo nazo hupitiwa na kuboreshwa pale inapobidi.
Kadhalika, utumishi wa umma nje unaongozwa na Mkataba wa Kimataifa
wa Vienna wa Mwaka 1961 kuhusu ushirikiano wa masuala ya kidiplomasia
na Mkataba wa Kimataifa wa Vienna wa Mwaka 1963 kuhusu masuala ya
kikonseli.
6.4 Katika kutekeleza jukumu la Wizara la kusimamia haki na kinga za
wanadiplomasia hapa nchini, Wizara inaongozwa na Sheria ya Haki na
Kinga za Kidiplomasia, Na. 5 ya Mwaka 1986 (Diplomatic and Consular
Immunities and Privilege Act (CAP 356 R.E. 2002). Pia katika kusimamia
Taasisi na Mashirika ya Kikanda na Kimataifa Wizara inaongozwa na
Mikataba ya Uenyeji kati yake na taasisi au mashirika hayo.
6.5 Sheria nyingine inayosimamiwa na Wizara inahusu usimamizi wa
mipaka ya kimataifa ya bahari ya mwaka 1989 (The Territorial Sea and
Exclusive Economic Zone Act (CAP 238 R.E. 2002).
25
7.0 MABADILIKO NA MATUKIO MAKUU KATIKA MFUMO
WA KISIASA, KIULINZI, KIUTAWALA, KIUCHUMI,
KITEKNOLOJIA NA KIJAMII
7.1 Kama ilivyoelezwa awali katika Taarifa hii, mabadiliko mbalimbali
ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na mengineyo ndani na nje ya nchi
yamechangia kwa kiasi kikubwa kubadilika kwa sera, muundo, na kupanuka
kwa majukumu ya Wizara. Hivyo sehemu inayofuata inaelezea mabadiliko
na matukio hayo. Miundo ya Wizara ya 2006 na 2010 imo katika taarifa hii.
7.2 Hatua ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ya kujiuzulu nafasi ya
Waziri Mkuu tarehe 22 Januari 1962, ikiwa ni miezi michache tu baada ya
uhuru wa Tanzania Bara na kuamua kwenda kuimarisha chama cha TANU,
ilikuwa ni moja ya matukio ya nadra ambayo yaliwashtua wananchi na
ulimwengu kwa sababu haikutegemewa kutokea.
7.3 Matukio mengine makuu yaliyofuata baada ya uhuru yalikuwa ni
pamoja na:
7.3.1. Kupatikana kwa Jamhuri ya Tanganyika tarehe 9 Disemba, 1962
kuliiondoa rasmi nchi yetu kutoka kwenye mamlaka ya Malkia wa
Uingereza;
7.3.2 Kuanzishwa kwa Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika (OAU) mnamo
mwaka 1963;
26
7.3.3 Tukio la tarehe 17 Januari 1964 la uasi wa Jeshi (Kings African
Rifles) lililokuwa limerithiwa kutoka kwa wakoloni dhidi ya Serikali
ya Tanganyika uliopelekea kufutwa kwa jeshi hilo na badala yake
likaanzishwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania;
7.3.4 Muungano kati ya Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa
Zanzibar tarehe 26 Aprili, 1964 na kuzaliwa kwa Taifa jipya lililoitwa
Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na baadaye kuitwa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
7.3.5 Kuvunja uhusiano wa kidiplomasia na Ujerumani Magharibi mwaka
1965 kutokana na Serikali hiyo kutaka tusiitambue Serikali ya
Ujerumani Mashariki; na
7.3.6 Kuvunja uhusiano wa kidiplomasia na Uingereza mwaka 1965
kutokana na Serikali hiyo kuitambua Serikali ya kidhalimu ya Ian
Smith.
7.3.7 Kuzaliwa kwa Azimio la Arusha la tarehe 5 Februari, 1967 lililoweka
njia kuu za uchumi wa Tanzania kuwa mikononi mwa umma wa
Watanzania;
7.3.8 Kuundwa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka 1967 iliyokuwa
imeundwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jamhuri ya Kenya
na Jamhuri ya Uganda ili kuimarisha huduma za kijamii na kiuchumi.
Jumuiya hiyo ilivunjika mwaka 1977 na kudhoofisha ushirikiano wa
kijamii na kiuchumi uliokuwa umejengeka katika nchi hizo. Hata
27
hivyo, tarehe 7 Julai 2000, wanachama waasisi walianzisha tena
Jumuiya ya Afrika Mashariki.
7.3.9 Kuunganishwa kwa vyama vya TANU na Afro-Shiraz Party (ASP)
tarehe 5 Februari, 1977 na kuzaliwa kwa Chama cha Mapinduzi
(CCM);
7.3.10 Kuanzishwa kwa Chuo cha Diplomasia kilichopo Dar es Salaam
mwaka 1978 kwa ushirikiano wa Tanzania na Msumbiji
kulikoimarisha ushirikiano na mahusiano ya nchi hizo mbili na nchi
nyingine;
7.3.11 Vita dhidi ya Iddi Amin wa Uganda iliyoanza tarehe 4 Novemba,
1978 na kumalizika Julai, 1979 ilidhoofisha mahusiano ya nchi yetu
na Uganda kwa wakati huo na kuathiri uchumi wa Taifa letu;
7.3.12 Mabadiliko ya mfumo wa kiuchumi kutoka uchumi wa kuhodhiwa na
dola kwenda uchumi huria;
7.3.13 Kuanzishwa upya kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini
mwaka 1992 ili kupanua demokrasia na ushindani wa kisiasa;
8.0 MAFANIKIO YALIYOPATIKANA HADI SASA
8.1 Mara baada ya Wizara kuundwa mwaka 1963, changamoto kubwa
ilikuwa ni kuandaa sera ya mambo ya nje kulingana na hali ya kipindi kile,
kuajiri watumishi wenye sifa ili kuchukua nafasi zilizoachwa wazi na
28
wakoloni, na kufungua ofisi za uwakilishi nje ya nchi ili kuongeza ufanisi
wetu wa kujishughulisha na mambo ya nje.
8.2 Baadhi ya masuala yote hayo yalitafutiwa ufumbuzi wa haraka na
mengine kuwekwa katika mipango ya muda mrefu. Moja ya mipango ya
haraka ilikuwa Afrikanaizesheni yaani, kuwapa wazalendo nafasi za kazi
zilizokuwa zikishikiliwa na raia wa kigeni. Mwaka 1964, Waraka wa Rais
Na. 2 uliweka kanuni na malengo ya msingi ya sera ya mambo ya nje ya
Tanzania. Kadri miaka ilivyokwenda, ofisi za uwakilishi zilifunguliwa
katika nchi mbalimbali duniani kwa kuzingatia umuhimu na maslahi ya nchi.
8.3 Kutokana na kuwa na sera ya mambo ya nje yenye misingi na
malengo madhubuti, Wizara imeweza kushiriki kikamilifu katika uwanja wa
diplomasia na maendeleo ya nchi tangu ilipoanzishwa. Tangu kipindi hicho,
sauti ya Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje imepaa katika medani za
kikanda na kimataifa na kuiletea sifa na heshima kubwa nchi yetu katika
harakati mbalimbali zikiwemo kutetea haki ya wanyonge, kudai usawa,
kupigania uhuru, kuendeleza mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi,
kuhimiza mshikamano barani Afrika, na kudumisha siasa ya kutofungamana
na upande wowote. Hakika, misingi imara ya serĂ¡ ya mambo ya nje
kumeifanya Tanzania kupata mafanikio ya jumla na kuipa mamlaka ya
kidiplomasia zaidi ya uwezo wake kiuchumi.
8.4 Tangu ilipoanzishwa, Wizara imejishughulisha sana kwa kushirikiana
na nchi Nne zilizokuwa katika kundi la Mstari wa Mbele (Tanzania, Zambia,
Botswana na Nigeria), pamoja na vyama vya ukombozi vya ANC cha Afrika
Kusini, FRELIMO ya Msumbiji, ZAPU ya Zimbabwe, MPLA ya Angola na
SWAPO ya Namibia katika ukombozi kusini mwa Afrika. Jitihada za nchi
29
hizo zilipelekea kupatikana kwa uhuru katika nchi za Msumbiji mnamo
mwezi Juni 1975; Angola mwezi Novemba 1975; Zimbabwe mwezi Aprili
1980; Namibia mwezi Machi 1990; na kukomesha sera za ubaguzi wa rangi
nchini Afrika Kusini mwezi Februari 1990. Ilipofika mwezi Mei, 1994
Afrika Kusini ilipata Rais wa kwanza mzalendo Mzee Nelson Mandela.
8.5 Katika kuendeleza umoja na mshikamano barani Afrika, Wizara yetu
imeshiriki kikamilifu katika majadiliano hadi kufikia Umoja wa Nchi Huru
za Kiafrika (OAU) ulioundwa 25 Mei 1963. Taasisi hiyo imekuwa mstari wa
mbele kupiga vita ukoloni na kuimarisha mshikamano katika masuala
mbalimbali yanayohusu nchi za Afrika. Baada ya kukamilisha jukumu
kubwa la wakati ule, Taasisi hiyo imefanya mageuzi katika miaka ya tisini
ili kukabiliana na changamoto zilizopo duniani.
8.6 OAU na sasa AU ina faida nyingi kwa nchi yetu, iliyo wazi ni ile ya
kudumisha amani, usalama na utatuzi wa migogoro barani Afrika. Aidha,
Taasisi imekuwa mstari wa mbele katika kuratibu msimamo wa Afrika na
kuimarisha sauti ya pamoja katika masuala mbalimbali yenye maslahi kwa
bara letu. Shabaha ya baadaye ya Umoja wa Afrika ni kufikia hatua ya
kuwa na Serikali moja ya Afrika. Hata hivyo, kuna safari ndefu kufikia
hatua hiyo.
8.7 Kwa kuzingatia ushiriki kamilifu wa Tanzania katika Umoja huo, nchi
yetu imepata heshima ya kuongoza OAU na baadaye AU kwa vipindi viwili
tofauti, yaani mwaka 1984 - 1985 na 2008. Katika vipindi hivyo, Tanzania
ilipata fursa nzuri ya kutoa mchango wake katika kufikia malengo ya Umoja
huo. Zaidi ya hapo, Tanzania iliweza kupata heshima kubwa baada ya raia
wake na wanadiplomasia mahiri kuchaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa Umoja
30
wa Afrika kwa muda wa miaka kumi kati ya 17 Julai, 1989 hadi 17
Septemba, 2001. Tanzania inaendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli
za Umoja wa Afrika na kupambana na changamoto zinazoukabili ili
kuufanya Umoja huo uwe na faida zaidi, hususan katika kutafuta jawabu la
changamoto za maendeleo zinazolikabili bara la Afrika.
8.8 Kwa muktadha huo, Tanzania imeendelea kuunga mkono juhudi zote
za Umoja wa Afrika zinazolenga kuhakikisha kuwa bara la Afrika
linachukua nafasi stahiki ulimwenguni katika masuala muhimu ya kiuchumi,
kijamii na kisiasa. Hivyo, Tanzania imeendelea kutetea msimamo wa Afrika
unaotaka usawa na uwazi katika biashara ya kimataifa. Pia, Tanzania
inaunga mkono jitihada za bara la Afrika za kufikia malengo ya millenia
ifikapo mwaka 2015 kwa kuhimiza nchi wahisani kuongeza ushirikiano
katika kukabiliana na changamoto zilizopo.
8.9 Kwa upande wa mazingira, Tanzania inaunga mkono na kutetea
msimamo wa Afrika wa kudai msaada zaidi kutoka nchi za magharibi ili
bara la Afrika liweze kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi
yanayotishia ustawi na utulivu wa jamii barani Afrika na kwingineko
duniani. Aidha, Tanzania ipo mstari wa mbele na inaunga mkono hoja ya
utangamano wa bara la Afrika kupitia jumuiya za kikanda. Hivyo, msisitizo
wa Tanzania ni kuimarisha jumuiya za kikanda ili hatimaye ziweze
kuchochea dhamira ya kufikia serikali moja ya Afrika. Zaidi ya hapo,
Tanzania inahimiza na kuunga mkono juhudi za kudumisha ushirikiano
baina ya Afrika na washirika wa maendeleo kama vile Umoja wa Ulaya;
China; India; Uturuki; Amerika Kusini; Korea Kusini nakadhalika.
31
8.10 Kuhusu ulinzi na usalama, Tanzania imekuwa ikishiriki na kuunga
mkono juhudi zote zinazolenga kutatua migogoro na kudumisha amani
barani Afrika. Pamoja na kushiriki katika usuluhishi wa migogoro
mbalimbali, Tanzania imeafiki, kuunga mkono na kushiriki katika mchakato
wa uundwaji wa Jeshi la Afrika. Aidha, Tanzania inaendelea kutoa askari
wake ili kushiriki katika vikosi vya kulinda amani barani Afrika. Katika hilo,
Tanzania imewahi kushiriki katika zoezi la kulinda amani kwenye nchi za
Liberia; Sierra Leone; Shelisheli; Comoro; na Sudan.
8.11 Sanjari na hilo, Tanzania inaunga mkono juhudi za kuimarisha
demokrasia, haki za binadamu na utawala bora. Katika kutekeleza hili,
Tanzania imeridhia mikataba yote ya Umoja wa Afrika inayolenga
kuimarisha demokrasia, haki za binadamu na utawala bora. Hatua hii ni
pamoja na kuanzisha programu ya kitaifa ya kujitathmini wenyewe ya
APRM. Pia, Tanzania inaendelea kushiriki katika uangalizi wa chaguzi
mbalimbali barani Afrika. Lengo kubwa la ushiriki wake katika suala hili ni
kuunga mkono jitihada za kuimarisha demokrasia.
8.12 Aidha, Tanzania imekuwa mstari wa mbele katika michakato ya
kuanzisha asasi mbalimbali za umoja wa Afrika kama vile: Bunge la Afrika,
Mahakama ya Afrika; Baraza la Usalama la Afrika na nyinginezo zote
zikiwa na shabaha ya kuimarisha, kudumisha na kulinda haki, usawa na
amani.
8.13 Katika kuunga mkono haja ya kudumisha utamaduni wa Afrika,
Tanzania imefanikiwa kutetea lugha ya Kiswahili kutambuliwa rasmi ili
itumike katika shughuli zake. Inatia moyo kuwa hivi sasa lugha ya Kiswahili
inatambuliwa na Umoja wa Afrika. Hatua kadhaa zinachukuliwa ili lugha
32
hiyo ianze kutumika rasmi katika shughuli za kila siku za Taasisi hiyo.
Aidha, Watanzania kadhaa wenye sifa wamejitokeza na kupewa nafasi ya
kutumikia Umoja wa Afrika katika nafasi na nyadhifa mbalimbali.
8.14 Katika kuhakikisha kuwa nchi maskini na zinazoendelea zinakuwa na
sauti moja katika kudai maslahi yake, Tanzania imeshiriki kikamilifu katika
mikutano mingi ya kimataifa inayotafuta msimamo wa pamoja wa nchi
maskini za duniani katika kulinda na kutetea haki zao. Hii ilikuwa ni pamoja
na kuanzishwa kwa Kundi la Nchi 77 na China. Katika kutetea haki za
wanyonge na usawa, Tanzania haikusita kuitetea China kuwa mwanachama
wa Umoja wa Mataifa na hatimaye kuwa Mjumbe wa Kudumu wa Baraza la
Usalama la Umoja wa Mataifa. Wakati wote, Wizara imetimiza kikamilifu
jukumu la kuratibu ushiriki wa Tanzania na pia kushiriki katika majadiliano
husika katika Umoja wa Mataifa.
8.15 Jambo lingine ambalo nchi yetu inajivunia ni ushiriki katika shughuli
za Umoja wa Mataifa katika jitihada zake za kuimarisha maendeleo ya
uchumi wa kimataifa, amani na usalama. Katika Umoja huo, Tanzania
imetamka waziwazi msimamo wetu katika mambo yote yanayohusu usawa
wa binadamu, ukoloni, na maendeleo ya nchi changa. Kwa kuheshimu
mchango wa Tanzania, nchi yetu ilipewa heshima ya kuwa Mwanachama wa
Muda wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa katika vipindi viwili
tofauti yaani mwaka 1975 na mwaka 2006, na Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa iliweza kutumia vyema fursa hizo.
8.16 Aidha, Wizara imefanikisha Watanzania kadhaa kushika nyadhifa
mbalimbali za uongozi wa juu na za kawaida katika ofisi za Umoja wa
Mataifa na mashirika yake. Matarajio ya Wizara ni kuongeza idadi ya
33
Watanzania kushika nafasi hizo, hususan baada ya kuundwa kwa Idara
inayoshughulikia masuala hayo.
8.17 Mnamo mwaka 1978, Tanzania ilikuwa mwenyeji wa Mkutano wa
Mawaziri wa Kundi la Nchi 77 na China uliofanyika mjini Arusha. Kwa
kutambua mchango wake, Tanzania ilipewa jukumu la kuwa Mwenyekiti wa
Kundi la Nchi 77 na China mwaka 1998 ambapo iliifanya kazi hiyo kwa
ufanisi mkubwa.
8.18 Tanzania, kwa kushirikiana na wanachama wengine waliomo kwenye
kundi hilo, ilikuwa mstari wa mbele katika kuunda Kamisheni ya Nchi za
Kusini na hatimaye Kituo cha Nchi za Kusini. Juhudi zote hizi ni
kuhakikisha kuwa sauti ya nchi maskini inasikilizwa na maslahi yao
yanapewa kipaumbele na jumuiya ya kimataifa, na Wizara yetu imekuwa
kiungo muhimu katika kuratibu na kushiriki katika juhudi zote zilizorejewa
katika masuala haya.
8.19 Tanzania imekuwa na msimamo wa kuendeleza siasa ya
kutofungamana na upande wowote. Katika hili, Tanzania imepata mafanikio
makubwa, hususan katika kipindi kile cha vita baridi baina ya nchi za
Mashariki na Magharibi. Juhudi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano
wa Kimataifa imefanikisha Nchi yetu kuweza kuwa rafiki wa nchi
mbalimbali kutoka kila upande, ili mradi waliheshimu utu wetu na kutambua
misingi ya usawa wa binadamu. Hiyo ilikuwa hatua kubwa kutoka hali
tuliyoachiwa na serikali ya kikoloni ya Uingereza ya kuambatana na upande
wa Magharibi peke yake.
34
8.20 Wizara imeendelea kudumisha na kuimarisha mafanikio haya hata
baada ya kuhuisha sera yake ya mambo ya nje mnamo mwaka 2001. Hii
inatokana na ukweli kuwa japokuwa sera mpya inaweka mkazo kwenye
malengo ya uchumi, hususan kukuza ushirikiano wa kiuchumi na wabia wa
maendeleo, lakini inaendelea kudumisha misingi mikuu ya sera ya awali ya
mambo ya nje kama ilivyokwisha elezwa hapo awali katika Taarifa hii.
Hivyo, Wizara inaendelea kupata mafanikio katika kulinda uhuru wa
kujiamulia mambo ya nchi yetu; kudumisha ujirani mwema; kuendeleza
Umoja wa Afrika; Kuunga mkono Umoja wa Mataifa; kuunga mkono
utekelezaji wa sera ya kutofungamana na upande wowote; na kuheshimu
haki za binadamu na usawa.
8.21 Rekodi nzuri ya Tanzania katika masuala ya kutetea haki za binadamu
na usawa sasa inafahamika ulimwenguni kote. Kwa kuzingatia hilo, mnamo
mwaka 2006 Umoja wa Afrika uliichagua Tanzania kuwa makao makuu ya
Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu. Mahakama hiyo ipo
mjini Arusha. Vilevile wapo Watanzania kadhaa ambao wamechaguliwa au
kuteuliwa kushika nyadhifa za juu katika taasisi mbalimbali za kimataifa na
kikanda zinazojihusisha na masuala ya haki za binadamu.
8.22 Tanzania imekuwa mstari wa mbele katika kudumisha ujirani mwema
na nchi jirani. Muungano wa Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa
Zanzibar uliimarisha dhana ya ujirani mwema na kufungua ukurasa mpya
wa ushirikiano ambao unadumu mpaka leo. Muungano unazidi kuimarika
mwaka hadi mwaka na unatoa tumaini kuwa Afrika inaweza kuungana na
kuwa nchi moja. Mkakati wa ujirani mwema umekuwa na faida kubwa
kwani umetoa fursa mbalimbali za kiuchumi, kijamii na kiutamaduni baina
ya nchi yetu na majirani zetu. Ikiwa imepakana na nchi zipatazo kumi, na
35
kwa kutambua umuhimu wa nchi jirani, Tanzania Bara mara baada ya uhuru
ilianza kuimarisha ujirani mwema kikamilifu kupitia jitihada mbalimbali.
Kwa mfano, barabara ya lami yenye urefu kwa kilomita 105 kutoka Arusha
hadi Namanga ilijengwa na kukamilika mwaka 1967 kwa lengo la
kuimarisha mawasiliano kati ya Kenya na Tanzania.
8.23 Hivi sasa Tanzania na Kenya zimeunganishwa na barabara nyingi,
zikiwemo za Moshi – Himo – Tarakea hadi Taveta nchini Kenya. Aidha,
kuna barabara itokayo Tanga kwenda Mombasa kupitia mpaka wa
Horohoro, na nyingine itokayo Tarime hadi Kenya kupitia mpaka wa Sirari.
Zaidi ya hapo, Tanzania Bara na Uganda zinaunganishwa na barabara
itokayo Bukoba kwenda Masaka nchini Uganda.
8.24 Hali kadhalika, jitihada zimefanywa ili wananchi wa mipakani
watumie umeme kutoka Uganda, kama ilivyo kwa wananchi wa mpaka wa
Tanzania Bara na nchi ya Zambia. Pia biashara ya bidhaa na huduma katika
mipaka yetu imeshamiri ikiwa ni pamoja na mahusiano ya watu.
8.25 Kwa upande wa Burundi na Rwanda, jitihada za kuunganisha nchi
yetu na nchi hizo zilifanywa ikiwa ni pamoja na kujenga barabara ya
Rusumo – Lusahunga na daraja la Rusumo katika mto Kagera. Aidha,
Jumuiya ya pamoja iliyojulikana kama “Kagera Basin Organization”
ilianzishwa kwa madhumuni ya kuwaunganisha wananchi wa Tanzania
Bara, Burundi, Rwanda na Uganda kufanya shughuli zao za kiuchumi na
kijamii. Hali kadhalika, bandari ya nchi kavu ilijengwa Isaka mkoani
Shinyanga ili nchi za Rwanda na Burundi ziweze kupata shehena zao kwa
urahisi zaidi.
36
8.26 Bandari nyingine ya nchi kavu ilijengwa katika eneo la bandari ya Dar
es Salaam kwa ajili ya shehena za Malawi. Pia, bandari za Mwanza na
Kigoma ziliimarishwa ili kurahisisha usafirishaji wa shehena za Uganda na
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Juhudi nyingine za kuimarisha ujirani
mwema ni ujenzi wa daraja la Umoja la Mtambaswala linalounganisha
Tanzania na Msumbiji. Daraja hilo lilizinduliwa mwezi Mei 2010. Hali
kadhalika, Tanzania imeendelea na jitihada za kuthibitisha mipaka yake na
majirani kwa njia ya majadiliano ili kuepuka migogoro isiyo ya lazima.
8.27 Katika kuendeleza jitihada hizo, Tume za Kudumu za Pamoja za
ushirikiano zilianzishwa. Makubaliano ya Tume hizo yamekuwa kichocheo
katika kuimarisha ushirikiano wa Tanzania na nchi jirani katika maeneo ya
kiuchumi, kijamii na kisiasa. Aidha, ziara mbalimbali zinazofanywa na
viongozi wa kitaifa na kuratibiwa na Wizara zimeimarisha sana ujirani
mwema na kuiletea manufaa nchi yetu.
8.28 Halikadhalika, Wizara imeratibu na kushiriki katika kuanzisha
jumuiya za ushirikiano za kikanda kama vile Jumuiya ya Afrika Mashariki
(EAC), Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC),
PTA/COMESA na Jumuiya ya Nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi.
8.29 Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyoundwa baada ya ile ya awali
kuvunjika imeendelea kuimarika kwa kasi na nchi wanachama wake sasa
wamefikia watano kutoka watatu wa awali. Wanachama wa Jumuiya hiyo ni
nchi za Tanzania, Uganda, Kenya, Rwanda, na Burundi. Jumuiya hiyo ina
zaidi ya watu milioni 122 na pato la taifa la jumla ya dola za kimarekani
zaidi ya milioni 47,000.00. Kutokana na fursa zinazopatikana katika EAC,
kama vile ukubwa wa soko, fursa za uwekezaji nakadhalika, baadhi ya nchi
37
za jirani zimeonesha dhamira ya kutaka kujiunga na Jumuiya hiyo yenye
lengo la kuunda shirikisho hapo baadaye.
8.30 Jumuiya ya SADC iliyoanza kama Klabu ya Mulungushi na baadaye
Kundi la Nchi za Mstari wa Mbele wa Ukombozi wa nchi za kusini mwa
Afrika nayo imepiga hatua kubwa katika kuimarisha ushirikiano wa nchi
wanachama katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii. Kwa hakika
Jumuiya hii yenye soko la watu takriban milioni 250 na pato la taifa la jumla
ya zaidi ya dola za kimarekani milioni 380,000.00 imesaidia kuimarisha
biashara baina ya nchi wanachama hasa kwa kuzingatia kuwa wakati wa
Taarifa hii inatayarishwa, tayari asilimia 85 ya bidhaa za nchi hizo zilipewa
nafuu ya kodi. Katika nchi 15 za Jumuiya hiyo ambazo ni Tanzania, Angola,
Botswana, DRC, Lesotho, Madagascar, Malawi, Mauritius, Msumbiji,
Namibia, Shelisheli, Afrika Kusini, Swaziland, Zambia na Zimbabwe.
8.31 Mnamo Oktoba, 2008 Wakuu wa Nchi na Serikali wa EAC, SADC na
COMESA walikubaliana kuanzisha Soko Huru la Pamoja kujumuisha
jumuiya zote tatu. Soko hili la pamoja litakuwa na watu zaidi ya milioni 530
na pato la taifa la jumla ya zaidi ya dola za kimarekani milioni 625,000.00.
Majadiliano ya kukamilisha agizo la viongozi wakuu yanaendelea
kufanyika.
8.32 Mafanikio ya jitihada za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania hayakuishia tu kwenye mapambano ya ukoloni na ubaguzi wa
rangi. Kwa kuelewa amani ni msingi wa maendeleo, mojawapo ya serĂ¡ yake
ya mambo ya nje ni kudumisha amani, usalama na utulivu katika nchi yetu
na nchi jirani. Hivyo Serikali yetu imejishughulisha kikamilifu katika
kutafuta suluhu ya migogoro ya kisiasa kwa njia ya amani katika nchi za
38
jirani na Afrika kwa ujumla. Nchi yetu imeshiriki kikamilifu katika kudhibiti
na kutatua migogoro katika nchi mbalimbali kama inavyofafanuliwa hapa
chini:
Shelisheli: Mwezi Agosti 1982 majeshi ya Tanzania kwa kushirikiana na
Serikali ya Shelisheli yalifanikiwa kuzima jaribio la mapinduzi
ua Mamluki dhidi ya Serikali ya nchi hiyo.
Burundi: Tanzania imeshiriki katika kuandaa mchakato wa kutafuta amani
nchini Burundi, baada ya nchi hiyo kukumbwa na mgogoro wa
kisiasa kufuatia kuuawa kwa Rais Melchior Ndadaye mwaka
1993. Tanzania iliandaa zaidi ya vikao 20 vya Wakuu wa Nchi za
Kanda kujadili jinsi ya kumaliza uhasama nchini Burundi. Katika
kutekeleza azma hiyo, Wakuu wa Nchi za Kanda walimteua
Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kuwa
msuluhisho wa mgogoro huo. Kufuatia kifo cha Mwalimu
Nyerere, nafasi hiyo ilichukuliwa na Rais Mstaafu wa Afrika
Kusini Mhe. Nelson Mandela. Juhudi za viongozi hao,
zilihitimishwa kwa kusainiwa kwa Mkataba wa Arusha wa
Amani Nchini Burundi na kuwezesha serikali ya mpito
kuzinduliwa.
Pamoja na kusainiwa mkataba huu, amani haikurejea nchini
Burundi: na mazungumzo yaliendelea chini ya Mhe. Jacob Zuma
huku Wizara ikiendelea kuratibu na kushiriki katika majadiliano
hayo. Matokeo ya majadiliano hayo yalipelekea kusainiwa kwa
mkataba wa kusitisha mapigano kati ya Serikali ya Mpito ya
Burundi na Kikundi cha CNDD-FDD chini ya uongozi wa Pierre
39
Nkurunzinza. Hatimaye kutokana na utekelezaji wa mkataba huu
Mhe. Pierre Nkurunzinza alichaguliwa kuwa Rais wa Burundi
mwaka 2005 na kupatikana kwa amani nchini humo.
Rwanda: Nchini Rwanda, Wizara iliiwezesha Tanzania kushiriki katika
kutafuta suluhu baada ya kutokea kwa mauaji ya kimbari mwaka
1994 na kusababisha wimbi kubwa la wakimbizi. Mazungumzo
kati ya iliyokuwa Serikali ya Rwanda chini ya marehemu Juvenal
Habyarimana na wapiganaji wa Rwandese Patriotic Front (RPF)
yaliyofanyika mjini Arusha hadi Mkataba wa Arusha kuhusu
amani nchini Rwanda ulipopatikana. Pamoja na kwamba RPF
ilipata ushindi kupitia mtutu wa bunduki, Serikali yake ilitumia
Mkataba wa Arusha kama msingi wa Katiba wa nchi hiyo.
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo: Serikali ya Tanzania pia ilishiriki
katika juhudi za kusitisha mapigano katika Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo (JKK), kufuatia uvamizi uliofanywa na
Rwanda na Uganda, mwaka 1997, kumng’oa aliyekuwa Rais wa
Zaire Marehemu Joseph Desire Mobutu Sese Seko. Uvamizi huo
ulisababisha mtafaruku mkubwa baada ya Rwanda na Uganda
kufarakana na Rais Laurent Desire Kabila, na kujaribu
kumwondoa madarakani. Rais kabila aliomba msaada, na
Angola, Namibia na Zimbabwe zilituma vikosi vyao kumnusuru
Kiongozi huyo na kusababisha mapigano makubwa. Hivyo,
Serikali ya Tanzania, ilishiriki katika majadiliano ya kuandaa
mkataba wa kusitisha mapigano nchini JKK na kuandaa
mazungumzo baina ya Wakongomani, yaliyofanyika Sun-City,
Afrika ya Kusini, na hatimaye kuwezesha uchaguzi kufanyika
40
nchini humo. Licha ya uchaguzi huo kufanyika, mwezi Agosti
2008, kulizuka mapigano makali Mashariki mwa JKK, baina ya
Majeshi ya Serikali na Kikundi cha CNDP, ambayo yalitishia
kuvuruga amani nchini humo. Kufuatia hali hiyo, Viongozi wa
nchi za Kanda ya Maziwa Makuu, walikutana Nairobi mwezi
Novemba 2008, na kumteua Mhe. Benjamin William Mkapa,
Rais wa awamu ya tatu, kujiunga na Mhe. Olusegum Obasanjo,
Rais Mstaafu wa Nigeria kusuluhisha mgogoro huo. Juhudi za
viongozi hao, zilifanikisha kupunguza uhasama baina ya JKK,
Rwanda na Uganda na kuimarisha amani katika eneo la Maziwa
Makuu.
Kenya: Serikali ya Tanzania pia ilitoa mchango mkubwa katika kutafuta
suluhu nchini Kenya, kufuatia mzozo uliozuka nchini humo, baada
ya matokeo ya uchaguzi wa Rais uliofanyika Desemba, 2007
kutangazwa. Rais Jakaya Kikwete, akiwa Mwenyekiti wa Umoja
wa Afrika, aliombwa kuingilia kati, na kusaidia kutatua mgogoro
huo kwa kuimarisha jitihada za usuluhishi za jopo la viongozi
mashuhuri lililomhusisha pia Mhe. Rais Mstaafu Benjamin W.
Mkapa. Jopo hilo lilikuwa chini ya Uenyekiti wa Mhe. Koffi
Annan, Katibu Mkuu Mstaafu wa Umoja wa Mataifa. Juhudi za
Mhe. Rais Jakaya Kikwete ziliwezesha muafaka kupatikana kati ya
Chama cha PNU na ODM kukomesha vurugu na mauaji na
hatimaye Serikali ya umoja wa Kitaifa kuundwa nchini Kenya.
41
Madagascar: Kufuatia mabadiliko ya uongozi ya mwezi Machi, 2009
kinyume na Katiba, nchi hiyo iliingia katika mgogoro mkubwa wa
kisiasa. Tanzania kwa kushirikiana na nchi wanachama wa SADC
imeendelea na jitihada za kutafuta suluhu ya mgogoro huo.
Sudan: Kutokana na juhudi zake katika kutatua migogoro na kujenga
ufungamano Barani Afrika, Rais Jakaya Mrisho Kikwete
alichaguliwa kwa kauli moja, kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa
Afrika kwa kipindi cha mwaka 2008. Katika nafasi hiyo, Mhe.
Kikwete alisaidia katika kusukuma mbele jitihada za kutafuta
amani nchini Sudan. Juhudi hizo zilikuwa zimekwama, kutokana
na Serikali ya Sudan kukataa kupokea vikosi mahuluti vya Umoja
wa Afrika na Umoja wa Mataifa, kwenda kuimarisha hali ya
usalama katika jimbo la Darfur. Rais Omar Al Bashir alibadili
kauli hiyo na kuruhusu vikosi hivyo kupelekwa, kufuatia ziara ya
Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete, aliyoifanya nchini Sudan,
mwezi Septemba 2008, na hivyo kupunguza vifo vya raia katika
jimbo la Darfur na kuwezesha utekelezaji wa Mkataba wa Amani
Kusini mwa Afrika kuendelea.
Comoro: Mwaka 2008, Serikali ya Tanzania pia ilitoa mchango mkubwa
katika kumaliza mgogoro ulioikumba Comoro, kufuatia Kanali
Mohamed Bacar, Kiongozi wa Kisiwa cha Anjouan kuasi na
kung’ang’nia madarakani baada ya kumaliza muhula wake wa
uongozi. Kufuatia hali hiyo, Rais Ahmed Abdallah Mohamed
Sambi aliomba msaada wa Umoja wa Afrika kusaidia kukomesha
uasi huo. JWTZ iliongoza juhudi za kumngo’a muasi huyo, kwa
42
kushirikiana na majeshi kutoka Sudan na Libya pamoja na
Senegal na hivyo kurejesha utawala wa kikatiba nchini Comoro.
Cote d’Ivoire: Machafuko ya kisiasa nchini humo yalitokea mwezi
Disemba, 2010 baada ya matokeo ya uchaguzi mkuu wa nchi
hiyo kutangazwa. Kufuatia hali hiyo, Tanzania iliteuliwa na
Umoja wa Afrika mwezi Januari, 2011 kuwa katika Jopo la
Usuluhishi wa mgogoro wa kisiasa wa nchi hiyo. Jopo hilo
lilikamilisha kazi yake mwezi Machi, 2011 na kukabidhi taarifa
yake kwa Baraza la Usalama la Afrika. Mapendekezo yote ya
Jopo yaliidhinishwa. Hata hivyo kutokana na kutotii maamuzi ya
Umoja wa Afrika, aliyekuwa Rais wa Nchi hiyo, aling’olewa
madarakani kwa kutumia nguvu za kijeshi mwezi Aprili 2011.
Zimbabwe: Zimbabwe iliingia katika matatizo, baada ya Serikali ya nchi
hiyo, kufumbia macho uvamizi wa mashamba ya Wazungu na
wananchi wa Zimbabwe uliofanyika kwenye miaka ya 1997. Hali
ilizidi kuzorota, kufuatia uchaguzi uliofanyika mwaka 2002,
ambapo Chama Tawala cha ZANU-PF nusura kishindwe na
Chama cha “Movement for Democratic Change (MDC)”. Baada
ya hali ya maisha kuzorota na vuta nikuvute ya muda mrefu
mwezi Machi 2007, Mhe. Rais Jakaya kikwete, akiwa
Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama wa Jumuiya
ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) aliitisha
kikao kisichokuwa cha kawaida cha Asasi hiyo mjini Dar es
Salaam. Kikao cha Wakuu hicho, kilimteua Mhe. Thabo Mbeki,
aliyekuwa Rais wa Afrika ya Kusini kuwa msuluhishi wa
mgogoro wa Zimbabwe. Juhudi hizi hatimaye zilihitimishwa kwa
43
mkataba wa kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliyoingia
madarakani mwaka 2008. Pamoja na matatizo yanayoendelea
kuikabili Zimbabwe, Serikali ya Umoja wa Kitaifa imepunguza
uhasama uliokuwepo kati ya ZANU-PF na MDC, pamoja na
kuwezesha uchaguzi huru na haki kufanyika nchini humo mwezi
Machi, 2008. Aidha, Serikali hiyo imesaidia upatikanaji wa
chakula na kupunguza makali ya maisha kwa wananchi wa
Zimbabwe.
Kwa ujumla, hivi sasa hali ya usalama inaendelea kutengemaa
katika maeneo haya kuliko ilivyokuwa katika siku za nyuma.
Aidha, Demokrasia inaendelea kuimarika na vita vya wenyewe
kwa wenyewe vilivyokuwa vinatikisa nchi hizo sasa vinaelekea
kudhibitiwa. Katika baadhi ya nchi, Serikali za mseto zimeundwa
ili kupunguza uhasama wa kisiasa miongoni mwa vyama pinzani.
8.33 Mgogoro wa Somalia umechukua muda mrefu na unatishia usalama
wa nchi yetu na Afrika kwa ujumla. Tangu kupinduliwa kwa Rais wa nchi
hiyo mwaka 1991, hali ya usalama nchini humo imedorora sana na
wanamgambo wa al-Shaabab wanafanya ukatili wa hali ya juu dhidi ya raia
wasio na hatia. Kuzuka kwa maharamia katika pwani ya Somalia hadi katika
pwani zetu kunaathiri sana usalama na safari za meli katika eneo hilo.
Hivyo, Tanzania inaendelea kushiriki katika jitihada za kutafuta suluhu ya
mgogoro nchini humo kwa mashauriano ya viongozi wa nchi hiyo. Aidha,
Wizara inaendelea kushiriki kikamilifu katika majadiliano ya kutafuta
mstakabali wa Somalia yanayoratibiwa na International Contact Group.
44
8.34 Katika jitihada za kuimarisha ubia na nchi mbalimbali pamoja na
mashirika ya kimataifa, Wizara imeratibu ushiriki na kufuatilia matokeo ya
ziara za viongozi wa kitaifa katika nchi mbalimbali zenye lengo la kutafuta
misaada ya kiufundi na fedha; kutangaza fursa za uwekezaji; na
kuwashawishi watalii kutembelea Tanzania.
8.35 Hali kadhalika, viongozi mashuhuri wa mataifa mbalimbali na
mashirika ya kimataifa duniani walizuru Tanzania tangu enzi za uhuru.
Viongozi hao ni kama walivyooneshwa katika Jedwali Na. IV hapa chini:
Jedwali IV (Viongozi mashuhuri)
Na. Jina la Kiongozi Nchi/ Taasisi
1. Mfalme Haile Selassie Ethiopia
2. Rais Leonid Brezhnev Urusi
3. Rais Fidel Castro Cuba
4. Waziri Mkuu Cho En Lai Jamhuri ya Watu wa China
5. Rais Sekou Toure Guinea
6. Rais Nicolae Ceausescu Romania
7. Waziri Mkuu Indira Ghandhi India
8. Rais Gamal Abdul Nasser Misri
9. Rais Gaffar Mohamed el-
Nimeir
Sudan
10. Rais Milton Obote Uganda
11. Rais Iddi Amin Uganda
12. Rais Prof. Yusuf Lule Uganda
13. Rais Jomo Kenyatta Kenya
14. Rais Daniel Arap Moi Kenya
15. Rais Mohamed Ahmed Ben
Bella
Algeria
16. Rais Samora Machel Msumbiji
17. Rais Thomas Sankara Burkina Faso
18. Rais Josip Broz Tito Yugoslavia
19. Rais Askofu Makarios II Cyprus
20. Rais Erich Honecker Ujerumani Mashariki
21. Rais Albert Rene Shelisheli
45
22. Malkia Elizabeth II Uingereza
23. Rais Jimmy Carter Marekani
24. Rais Siad Barre Somalia
25. Rais Michael Norman Manley Jamaica
26. Rais Seretse Khama Botswana
27. Rais Michael Micombero Burundi
28. Rais Ketumire Masire Botswana
29. Rais Marien Ngouabi Congo
30. Rais Abdou Diouf Senegal
31. Rais Suharto Indonesia
32. Rais Yasser Arafat Palestine
33. Waziri Mkuu Olof Palme Sweden
34. Rais Jian Zemin Jamhuri ya Watu wa China
35. Rais Hu Jintao Jamhuri ya Watu wa China
36. Rais Kenneth Kaunda Zambia
37. Rais Frederick Chiluba Zambia
38. Rais Levy Mwanawasa Zambia
39. Rais Rupiah Banda Zambia
40. Rais Joachim Chissano Msumbiji
41. Rais Armando Emilio Guebuza Msumbiji
42. Rais Jomo Kenyatta Kenya
43. Rais Mwai Kibaki Kenya
44. Rais Yoweri Kaguta Museveni Uganda
45. Rais Nicolae Ceausescu Romania
46. Waziri Mkuu Dkt. M. Singh India
47. Rais Olusegun Obasanjo Nigeria
48. Rais Bill Clinton Marekani
49. Rais George W. Bush Marekani
50. Rais Sam Nujoma Namibia
51. Rais Hifikepunye Pohamba Namibia
52. Rais Ahmed A. M. Sambi Comoro
53. Rais Robert Mugabe Zimbabwe
54. Rais Nelson Mandela Afrika Kusini
55. Rais Thabo Mbeki Afrika Kusini
56. Rais Jacob Zuma Afrika Kusini
57. Rair Joseph Mobutu Seseseko Zaire (sasa Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Watu wa
46
Kongo)
58. Rais Laurent Kabila Jamhuri ya Kidemokrasi ya
Watu wa Kongo
59. Rais Joseph Kabila Jamhuri ya Kidemokrasi ya
Watu wa Kongo
60. Rais Festus Mogae Botswana
61. Rais Juvenal Habyarimana Rwanda
62. Rais Paul Kagame Rwanda
63. Rais Pierre Nkurunzinza Burundi
64. Rais Cyprien Ntaryamira Burundi
65. Rais Pierre Buyoya Burundi
66. Rais Kamuzu Banda Malawi
67. Rais Bakili Muluzi Malawi
68. Mfalme Mswati II Swaziland
69. Rais Jerry Rawlings Ghana
70. Kansela Helmut Kohl Ujerumani Magharibi
71. Papa John Paul II Vatican
72. Rais Mary Robinson Ireland
73. Rais Lula da Silva Brazil
74. Mhe. Kofi Annan Katibu Mkuu wa Umoja
wa Mataifa
75. Mhe. Ban Ki-moon Katibu Mkuu wa Umoja
wa Mataifa
76. Mhe. Asha Rose Migiro Naibu Katibu Mkuu wa
Umoja wa Mataifa
77. Waziri Mkuu Meres Zenawi Ethiopia
78. Rais Jose Dos Santos Angola
79. Rais Isaias Afewerki Eritrea
80. Rais Martti Ahtisaari Finland
81. Rais Gnassingbe Eyadema Togo
82. Waziri Mkuu Pakalitha
Mosilisili
Lesotho
* Chanzo: Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa na Idara ya Maelezo
47
8.36 Kutokana na ziara hizo, wafanyabiashara na wawekezaji kutoka nje
wanaendelea kuja Tanzania na kuwekeza au kuingia ubia na kufanya
biashara za pamoja na Watanzania katika sekta mbalimbali.
8.37 Moja ya mafanikio ambayo yanaonyesha kuimarika kwa ubia na nchi
mbalimbali ni ziara ya Rais George W. Bush wa Marekani. Mafanikio ya
ziara hiyo iliyofanyika mwezi Februari, 2008 ni pamoja na kuwekwa saini
Mkataba wa Maendeleo ya Milenia (Millennium Challenge Compact). Chini
ya Mkataba huo, Marekani inaipatia Tanzania jumla ya dola za Kimarekani
milioni 698 kwa kipindi cha miaka mitano. Fedha hizo zinatumika katika
uimarishaji wa miundombinu hususan barabara, umeme na huduma za
kijamii.
8.38 Aidha, mafanikio ya kuridhisha yamepatikana katika kuzishawishi
nchi wahisani kuongeza misaada yao kwa nchi yetu. Kwa mfano, mwezi
Machi, 2007 Japan ilisaini mikataba ya mkopo wa utekelezaji wa
MKUKUTA wa dola za Kimarekani milioni 20 utakaotolewa kila mwaka
kwa miaka mitano; mkopo wa shilingi bilioni 74.2 kwa ajili ya ujenzi wa
barabara ya Arusha-Namanga pamoja na uboreshaji wa huduma za uhamiaji
na forodha mpakani Namanga. Aidha, Serikali ya Japan imetoa ruzuku ya
dola za kimarekani bilioni 1.2 ili kugharamia miradi ya afya, maji, elimu na
biashara nchini na kutangaza hatua ya kuisamehe Tanzania deni la shilingi
bilioni 742.
8.39 Hali kadhalika, Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China imeahidi
kufuta madeni yote ambayo nchi hiyo inaidai Tanzania na pia kufufua
miradi yote iliyoanzishwa miaka ya sitini na sabini, hususan Reli ya
TAZARA, Kiwanda cha Nguo cha Urafiki, Kiwanda cha Zana za Kilimo
48
(UFI), na kuanzisha vituo viwili vya kisasa ambapo kimoja kitakuwa cha
upasuaji wa moyo na kingine cha masuala ya kilimo. Mnamo Mei, 2007
ziara ya Rais Hu Jintao wa China ilifanikisha uwekaji saini wa makubaliano
ya kujenga ukumbi wa mikutano wa Kimataifa jijini Dar es Salaam wa
Julius Nyerere International Convention Centre. Ujenzi huo umeanza na
utakamilika ifikapo mwezi Aprili mwaka 2012 .
8.40 Pia, majadiliano yanaendelea kati ya Tanzania na Brazil kwa
lengo la kufutiwa deni la kiasi cha dola za kimarekani 236,996,036.19
lililotokana na mkopo kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kiwango cha
lami kutoka Morogoro hadi Dodoma. Vilevile majadiliano yameanza
kati ya Tanzania na Iran ya kufutiwa deni la mafuta ambalo hadi
kufikia mwishoni mwa mwaka Septemba 2010 ilifikia kiasi cha dola
za kimarekani milioni 345,885,366.58.
8.41 Aidha, ni jambo la kushukuru kuona baadhi ya nchi washirika wa
maendeleo zimeifutia na zinaendelea kuifutia au kuipunguzia madeni nchi
yetu. Kwa mujibu wa taarifa kutoka Hazina nchi zilizofuta deni lao lote kwa
Tanzania ni: Uholanzi, Canada, Uingereza, Norway, Japan na Marekani.
Nchi ambazo zimefuta sehemu ya deni lao ni: Austria, Ubelgiji, Ufaransa,
Urusi, Ujerumani, Italia, Slovak/Czech (sasa Jamhuri ya Slovakia na ya
Czech), Bulgaria na India.
8.42 Aidha, India imeipatia tena nchi yetu mkopo wenye masharti nafuu
wa dola za kimarekani milioni 40 kwa ajili ya pembejeo za kilimo. Aidha,
Tanzania ilisaini mkopo mwingine na nchi hiyo wenye masharti nafuu wa
dola za kimarekani milioni 36 kwa ajili ya magari. Nchi hiyo pia imeahidi
kuongeza idadi ya nafasi za masomo ya juu kwa Watanzania katika fani
49
mbalimbali. Vilevile, kampuni ya TATA imeeleza nia yake ya kuwekeza
katika uchimbaji wa mafuta na gesi katika mkoa wa Mtwara.
8.43 Chini ya Mchakato wa Helsinki, Serikali za Tanzania na Finland
ziliamua kuanzisha nchini Tanzania taasisi ya Maendeleo Endelevu (The
Institute for Sustainable Development) ambapo Finland iliahidi kutoa Euro
milioni 8 kugharamia uendeshwaji wake kwa kipindi cha miaka minne.
Taasisi hiyo ilizinduliwa rasmi na Waziri Mkuu wa nchi hiyo alipofanya
ziara hapa nchini mwezi Machi 2010. Serikali za Tanzania na Finland
ziliamua kuunganisha Taasisi hii iliyokuwa inasimamiwa na Wizara na
Taasisi ya Uongozi iliyokuwa ianzishwe chini ya Ofisi ya Rais, Menejimenti
ya Utumishi wa Umma. Kuunganishwa kwa Taasisi hizi kumepelekea
kuanzishwa kwa Taasisi ya Uongozi na Maendeleo Endelevu Afrika iliyopo
Dar es Salaam, Tanzania.
8.44 Katika kuunga mkono jitihada za Umoja wa Mataifa za kuimarisha
maendeleo ya uchumi wa kimataifa, amani, na usalama, Wizara imeendelea
kushiriki kikamilifu katika mijadala ya kuleta mageuzi katika Umoja wa
Mataifa hususan katika Baraza la Usalama ili Afrika ipatiwe viti viwili vya
kudumu vyenye kura ya turufu. Mjadala huu ni mgumu na utachukua muda
mrefu kufikia makubaliano.
8.45 Tanzania kwa kushirikiana na Denmark iliandaa rasimu ya kuunda
Kamisheni ya Umoja wa Mataifa kushughulikia ujenzi wa nchi zinazotoka
katika migogoro chombo ambacho kimeanza kazi yake katika nchi za
Burundi na Sierra Leone. Pia, Tanzania imeendelea kuunga mkono
mchakato wa mageuzi katika taasisi za fedha za kimataifa kama vile Benki
50
ya Dunia (World Bank) na Shirika la Fedha Kimataifa (IMF), ili nchi
masikini zipatiwe sauti katika kusimamia shughuli za taasisi hizo.
8.46 Katika kuimarisha diplomasia ya mikutano, Wizara imeendelea
kuimarisha Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha. Hali hiyo
imewezesha Kituo hicho kuwa mwenyeji wa mikutano mingi mikubwa ya
kikanda na kimataifa ikiwa ni pamoja na ule wa Sullivan uliofanyika mwezi
Aprili 2008, TICAD-IV uliofanyika mwezi Mei, 2010. Aidha, Kituo
kimeendelea kutumika kwa ajili ya mikutano ya Jumuiya ya Afrika
Mashariki. Hali kadhalika, Wizara iliratibu kwa ufanisi mkubwa mkutano
wa Jukwaa la Uchumi Duniani (World Economic Forum) uliofanyika Dar es
Salaam, mwezi Mei 2010.
8.47 Mafanikio mengine katika kuimarisha ushirikiano wa pande mbili
baina ya nchi ni ufunguzi wa balozi mbalimbali katika nchi za nje. Hivi sasa
Tanzania ina balozi 32; balozi ndogo tatu; Vituo viwili vya Biashara; na
Konseli za Heshima 17. Aidha Serikali kwa kupitia Wizara inamiliki
majengo yake yapatayo 90 nje. Kati ya hayo 22 ni ofisi za balozi, 20 ni
makazi ya balozi na 48 ni makazi ya maofisa. Hii imepunguza mzigo wa
kulipa kodi za pango. Orodha ya majengo ya ofisi za balozi na nyumba
zinazomilikiwa na Serikali nje ni kama inavyoonekana katika Jedwali Na.
V hapa chini:
8.48 Hadi sasa Wizara ina jumla ya watumishi 440, kati ya hao 268 wapo
Makao Makuu na 172 balozini.
51
9.0 CHANGAMOTO ZILIZOJITOKEZA
9.1 Tangu Wizara ianzishwe, imekuwa ikikabiliana na changamoto
mbalimbali katika kutekeleza sera ya mambo ya nje. Kwa ujumla
changamoto kubwa iliyoikumba Wizara na Serikali nzima baada ya uhuru
ilikuwa ni kukosekana kwa wataalam wazalendo wa kushika nafasi
mbalimbali zilizoachwa wazi na wakoloni. Kwa upande wa Wizara,
kukosekana kwa uwakilishi nje ya nchi na ukosefu wa wataalam, majengo
ya ofisi za balozi na makazi ya balozi na maafisa vilikuwa ni changamoto
kubwa. Aidha, changamoto zingine kwa kipindi cha mwanzoni hadi sasa ni
pamoja na:
9.2Changamoto kubwa kwa Wizara hivi sasa na huko nyuma imekuwa ni
mabadiliko makubwa na ya haraka katika nyanja mbalimbali duniani
ambayo yamekuwa yakitulazimisha kubadilisha mikakati yetu ya kisera.
Mabadiliko makubwa kuliko yote yalikuwa ni kumalizika kwa vita baridi
kati ya kambi ya nchi za kibepari na kambi ya nchi za kijamaa na kuzuka
kwa taifa moja lenye nguvu;
9.3Katika mazingira hayo inahitaji jitihada kubwa zaidi kwa Tanzania na
nchi za Kiafrika au hata pamoja na nchi zinazoendelea kupata sauti ya
pamoja ili kutetea maslahi ya Taifa letu, ya Afrika au ya nchi
zinazoendelea;
9.4Umuhimu wa kutambua na kuendelea kushirikiana na Umoja wa Afrika,
nchi zisizofungamana na upande wowote pamoja na Umoja wa Mataifa,
katika kutafuta mbinu na mipango ya kumaliza changamoto zinazotokea
duniani kama vile ugaidi, mihadarati, mabadiliko ya tabia nchi,
usafirishaji wa binadamu n.k.;
52
9.5Kuendelea kuhuisha Sera ya Mambo ya Nje ili iendane na mahitaji ya
wakati;
9.6 Kushirikiana na nchi jirani na kikanda katika kuweka mazingira ya
ustawi wa amani, usalama na utulivu wa kisiasa; na
9.7 Tatizo la uharamia katika Pwani ya Bahari ya Hindi na mwambao wa
Afrika Mashariki ambao unaathiri usalama wa nchi, wananchi na mali
zao na kupunguza kasi ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania.
9.8 Kufungwa kwa baadhi ya Balozi za Tanzania Nje katika miaka ya tisini
kulikotokana na hali mbaya ya uchumi. Hali hii ilizorotesha mahusiano
mazuri yaliyokuwa yamejengeka baina ya nchi hizo na pia kuliinyima
Tanzania fursa za kiuchumi.
10.0 MATARAJIO
10.1 Katika kipindi kijacho, matarajio ya Wizara ni kuendelea kusimamia
na kutekeleza diplomasia thabiti ambayo itachangia katika shughuli za
kiuchumi na kuwezesha mageuzi ya haraka na maendeleo endelevu ya
Tanzania. Katika kufanya hivyo, mambo yafuatayo yatapewa kipaumbele:
10.2 Kuhuisha Sera ya sasa ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001 pamoja na
Kanuni za Utumishi Nje ya Nchi ili ziendane na mahitaji ya wakati;
10.3 Ujenzi wa jengo la Wizara linaloendana na mahitaji ya kipindi
kijacho;
53
10.4 Kuendelea kuajiri na kuwajengea uwezo watumishi wa Wizara ili
waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi;
10.5 Kuwa na Idara kamili ya Sheria itakayoboresha utendaji na kutoa
mwongozo vizuri zaidi kwa Wizara kama ilivyo kwa Wizara nyingine za
Mambo ya Nje duniani;
10.6 Kushiriki vizuri zaidi katika kusimamia utekelezaji wa Mikataba
mbalimbali baina ya Tanzania na nchi/ taasisi zingine ili iweze kuleta faida
zilizokusudiwa;
10.7 Kushirikiana na mamlaka husika nchini kuharakisha mchakato wa
kubadilisha Sheria ya Uraia ili kuwawezesha Watanzania waliopo nje ya
nchi kuwa na uraia wa nchi mbili na hivyo kushiriki kikamilifu katika
shughuli za kuchangia maendeleo ya nchi yao. Pia, kuendelea kuwatafutia
Watanzania fursa za kazi katika mashirika na taasisi za kikanda na
kimataifa;
10.8 Kujenga chuo cha mafunzo ya diplomasia cha kisasa na chenye hadhi
ya kimataifa kulingana na mahitaji na changamoto za wakati, ikiwa ni
pamoja na kupanua wigo kwa kukiwezesha Chuo kutoa mafunzo kwa
Wabunge, Mawaziri, na viongozi wengine wa Serikali ili kuelewa vizuri
zaidi masuala yanayohusu diplomasia;
10.9 Ujenzi wa Mount Kilimanjaro International Convention Centre mjini
Arusha ili kukidhi mahitaji ya mikutano ya kimataifa;
54
10.10 Ujenzi wa makazi ya kudumu ya Mahakama ya Afrika ya Haki za
Binadamu na Watu, pamoja na nyumba za viongozi wake na kusaidia
Mahakama hiyo iwe na nguvu na mamlaka inayokusudiwa na hivyo
kuheshimika Barani Afrika na dunia nzima;
10.11 Kuendelea kutekeleza mpango wa Serikali wa ujenzi wa ofisi za
balozi, makazi ya balozi, nyumba za watumishi ubalozini na vitega uchumi
ili kupunguza gharama za kuendesha balozi zetu, kuongeza vyanzo vya
mapato na kujihakikishia usalama zaidi;
10.12 Kufungua ofisi za uwakilishi katika maeneo mengine yenye umuhimu
wa kiuchumi na masuala mengine;
10.13 Kukuza na kuendeleza lugha ya Kiswahili barani Afrika na duniani
kote;
10.14 Kushiriki katika kujenga mazingira wezeshi ndani na nje ili hatimaye
kuwa na Tanzania inayojitegemea kwa asilimia mia moja;
10.15 Kukuza ubia wa kimataifa na kuimarisha ushirikiano wa kikanda,
barani Afrika na wadau wengine wa maendeleo ili kuhakikisha kuwa
Tanzania inapata manufaa ya fursa za utandawazi;
10.16 Kuimarisha na kudumisha ujirani mwema kwa faida ya nchi yetu;
10.17 Kuendeleza amani, usalama na utulivu wa kisiasa pamoja na
ushirikiano wa kiuchumi kikanda; na
10.18 Kuendelea kuratibu jitihada za kushawishi nchi wadai kutufutia
madeni.
55
11.0 TAASISI ZILIZOPO CHINI YA WIZARA YA MAMBO YA
NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
11.1 Kituo Cha Mikutano cha Kimataifa (Arusha International
Conference Centre – AICC)
11.1.1 Kituo kilianzishwa kwa mujibu wa Sheria Mama ya Mashirika
ya Umma ya mwaka 1969 kupitia Notisi ya Serikali Na. 115 ya tarehe
28 Agosti 1978.
11.1.2 Kituo kinamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100, chini ya
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, ambapo usimamizi
wa shughuli zake za jumla upo chini ya Bodi ya Wakurugenzi. Shughuli za
kila siku zinasimamiwa na Mkurugenzi Mwendeshaji, akisaidiwa na Wakuu
wa Idara wanne ambazo ni Ofisi za Mkurugenzi Mwendeshaji; Idara ya
Mikutano na Masoko; Idara ya Miliki na Miradi; Idara ya Fedha na Utawala;
na Idara ya Hospitali.
11.1.3 Shabaha ya kuanzisha Kituo hiki ilikuwa ni pamoja na
kuendesha biashara ya mikutano na kukodisha ama kupangisha watu na
taasisi mbalimbali ofisi na nyumba zake. Aidha, Kituo kinamiliki hospitali
kwa ajili ya kutoa huduma kwa wafanyakazi na jamii kwa ujumla. Hospitali
hii ni chanzo kingine cha mapato cha Kituo.
11.1.4.1 Kauli mbiu ya AICC ambayo pia ni sehemu ya taswira ya Kituo ni
“We bring the world to Tanzania”.
56
Hali ya Uongozi na Utawala Tangu Ilipoanzishwa
11.1.5 Tangu kuanzishwa kwake mwaka 1978, Kituo kimekuwa chini ya
Wenyeviti wanane (8) wa Bodi ya Wakurugenzi kama inavyooneshwa
katika Jedwali Na. VI hapa chini:
Jedwali Na. VI (Bodi )
Na. Jina Muda wa Utumishi
1. Balozi Anthony B. Nyakyi Agosti 1978
2. Balozi Daniel Mloka 1979 – Julai 1981
3. Balozi Paul Rupia Julai 1984 - Julai 1986
4. Bw. Ashour A. Abbas Julai 1986- Aprili 1987
5. Bw. Abdu C. Faraji Julai 1987 - Machi 1991
6. Bw. Mustafa H. M. Mkulo Aprili 1991 - Juni 2005
7. Prof. Mwajabu K. Possi Julai 2006 - Juni 2009
8. Balozi Christopher C. Liundi Novemba 2009 - hadi sasa
11.1.6 Tangu kuanzishwa kwake, Wakurugenzi Waendeshaji saba
waliteuliwa kuongoza Kituo hicho kama inavyooneshwa katika Jedwali Na.
VIII hapa chini:
Jedwali Na. VII (Uongozi)
Na. Jina Muda wa Utumishi
1. Bw. Frank Mwanjisi Julai 1978 – Machi 1980
2. Bw. Sammy Mdee Aprili 1980 – Agosti 1989
3. Bw. Edward Lowassa Desemba 1989 – Desemba 1990
4. Balozi Daniel Mloka Aprili 1992 – Julai 1993
5. Meja Jenerali Mstaafu Herman
Lupogo
Novemba 1993 – Juni 2000
6. Bw. Patrick Tsere Julai 2002 – Agosti 2005
7. Bw. Elishilia Daniel Kaaya Aprili 2007 – hadi sasa
57
11.1.7 Kama ilivyoelezwa hapo juu, Kituo kiliundwa na Sheria ya
Mashirika ya Umma ya mwaka 1969. Hivyo, uendeshaji wa shughuli za
Kituo unazingatia maelekezo mbalimbali kutoka iliyokuwa Ofisi ya
Kuratibu Mashirika ya Umma (SCOPO) na sasa Msajili wa Hazina. Kituo
kimekuwa kikiendeshwa kwa kuzingatia sera mbalimbali zinazopitishwa na
Bodi ya Wakurugenzi kwa mujibu wa Sheria na Kanuni zilizopo.
Mafanikio ya Kituo
11.1.8 Kituo kimefanikiwa kuitangaza vyema nchi yetu na vivutio
vyake kupitia mikutano mbalimbali ya kitaifa, kikanda na kimataifa
ikiwemo ya Kundi la Nchi 77 na China (G -77); mikutano ya usuluhishi wa
mgogoro wa Burundi na Rwanda; mikutano ya Jumuiya ya Afrika
Mashariki; mkutano wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika, mwaka
2008; mkutano wa Sullivan, mwaka 2008; na mkutano wa Nne wa Kimataifa
wa Ushirikiano wa Afrika na Japan (TICAD-IV), mwaka 2010.
11.1.9 Mikutano hiyo imesaidia kuongeza fursa za ajira, utalii, mapato
kwa Serikali na wadau mbalimbali na pia kuchochea shughuli nyingine za
uchumi na biashara. Aidha, Kituo kimeweza kutoa ofisi kwa taasisi
mbalimbali za kimataifa kama vil e Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya
Kimbali ya Rwanda (ICTR), Jumuiya ya Afrika Mashariki, na Mahakama ya
Afrika ya Haki za Binadamu na Watu.
58
Changamoto Zilizojitokeza
11.1.10 Pamoja na mafanikio yaliyopatikana, Kituo kinakabiliwa na
changamoto kubwa mbili, ambazo ni uhaba wa kumbi za mikutano kwa vile
Kituo hakikujengwa mahsusi kwa ajili hiyo bali kuhudumia ofisi za Makao
Makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyovunjika 1977. Upungufu huu
unakiathiri Kituo na nchi kwa ujumla katika diplomasia ya mikutano na
utalii kwa ujumla. Changamoto nyingine ni ukosefu wa rasilimali fedha ili
kufanikisha ujenzi wa kituo cha kisasa kitakachokidhi mahitaji ya sasa na
pia kuweza kukabiliana na ushindani uliopo.
Matarajio ya Kituo kwa Kipindi Kijacho
11.1.11 Kituo kitaendelea na jitihada za kuitangaza Tanzania kupitia
mikutano mbalimbali. Aidha, inatarajiwa kuwa ujenzi wa ukumbi wa
mikutano wa kisasa wa Mount Kilimanjaro International Convention Centre
(MK-ICC) utakamilika ili kukidhi mahitaji ya mikutano. Vile vile,
inatarajiwa kuwa Kituo kitaanzisha vituo kadhaa vya aina hiyo katika mikoa
mingine ya Tanzania.
11.2 Chuo cha Diplomasia (Centre for Foreign Relations – CFR)
11.2.1 Chuo cha Diplomasia kina historia ndefu na ya kujivunia katika
kuchangia juhudi za maendeleo ya taifa letu. Chuo kilianzishwa mwaka
1978 kama mradi wa ubia kati ya Serikali mbili, yaani Serikali ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Msumbiji. Tangu
kuanzishwa kwake, Chuo kimejishughulisha na kutoa mafunzo na kufanya
59
tafiti katika nyanja za Diplomasia, Itifaki, Mahusiano ya Kimataifa, Lugha
za Kigeni, Stadi za Stratejia na Utatuzi na Usuluhishi wa Migogoro.
11.2.2 Shabaha ya kuanzishwa kwake ilikuwa ni kuwatayarisha
maafisa na watumishi wa Wizara husika za nchi wanachama. Katika kipindi
chote hicho, Chuo kimekua na kupanuka kukidhi mahitaji ya mafunzo na
huduma nyinginezo za kitaaluma kwa taasisi za Serikali, mashirika ya umma
na binafsi, Balozi mbalimbali na umma wa nchi hizo mbili kwa ujumla.
Historia ya Chuo
11.2.3 Chuo cha Diplomasia kinachotambulika rasmi kama “Tanzania
– Mozambique Centre for Foreign Relations”, kipo barabara ya Kilwa jijini
Dar es Salaam katika maeneo ya Kurasini. Chuo kimo katika eneo la
iliyokuwa Taasisi ya Msumbiji, (Mozambican Institute). Taasisi hii ilikuwa
ikimilikiwa na Chama cha Kupigania Uhuru wa Msumbiji, FRELIMO.
Taasisi ilitumika kuratibu harakati za ukombozi wa nchi hiyo. Baada ya
Msumbiji kupata uhuru wake mwaka 1975, majengo ya taasisi yaliachwa
bila shughuli wala matunzo yoyote.
11.2.4 Hivyo, ili kuendeleza mahusiano mema ya kindugu ya muda
mrefu, viongozi wa nchi za Tanzania na Msumbiji walibuni wazo la
kuanzisha Kituo cha Mahusiano ya Kimataifa (Tanzania - Mozambique
Centre for Foreign Relations). Lengo kuu lilikuwa ni kutoa mafunzo ya
diplomasia na mambo ya kimataifa kwa manufaa ya Serikali za nchi hizi
mbili na wananchi wake. Uamuzi wa uanzishwaji wa Chuo ulienda sanjari
na matumizi ya ardhi na majengo ya Taasisi ya Msumbiji. Uamuzi huo wa
kidiplomasia na kisiasa ulifuatiwa na makubaliano ya uanzishwaji wa chuo
60
yaliyofanyika tarehe 13 Januari, 1978 jijini Maputo yaliyotiwa saini na
waliokuwa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Mhe. Benjamin
William Mkapa na Mhe. Alberto Joachim Chissano wa Msumbiji.
Makubaliano hayo ndiyo yaliyotoa msingi wa Katiba ya Chuo.
11.2.5 Mwaka 1986, Serikali ya Tanzania ilipitisha Sheria ya Kinga na
Upendeleo wa Kidiplomasia, Sheria Na. 5 ya mwaka 1986. Sheria hiyo
ilikipa Chuo hadhi ya kidiplomasia. Aidha, Sheria hii ilikitambua Chuo
kama taasisi huru ya mafunzo na ilikipa Chuo mamlaka ya kupanua wigo wa
shughuli zake.
11.2.6 Kwa kipindi cha miaka mitano tangu kianzishwe, Chuo
kilifanikiwa kwa kiasi kikubwa kutekeleza majukumu yake kama taasisi ya
ubia. Nchi zote mbili zilishiriki katika uendeshaji wa Chuo. Baraza la Chuo
lilishirikisha wajumbe kwa idadi sawa toka pande zote mbili. Tanzania na
Msumbiji zilichangia sawa katika bajeti ya Chuo, na kila nchi ilipeleka
wanafunzi chuoni. Mafunzo kwa vitendo yalifanyika katika nchi zote mbili
kwa utaratibu uliokuwa umewekwa.
11.2.7 Kuanzia mwaka 1982, Msumbiji iliacha kuchangia bajeti ya
chuo na pia kushiriki katika shughuli za uendeshaji. Aidha, ilipunguza idadi
ya wanafunzi wake Chuoni. Hatimaye, Serikali ya Msumbiji ilianzisha chuo
chake, Institute Superor de Relacoes Internacionais (ISRI), kinachofanana
kwa majukumu na Chuo cha Diplomasia. Tangu wakati huo hadi hivi sasa,
Serikali ya Tanzania, kupitia Wizara ya Mambo ya Nje, imeendelea kubeba
majukumu ya kukiendesha na kugharamia shughuli zote za Chuo peke yake.
61
11.2.8 Baada ya kukabiliana na changamoto mbalimbali Baraza la
Chuo liliamua Chuo kifanye mabadiliko ya kuwa sehemu ya Chuo Kikuu
cha Dar es Salaam. Hatimaye mwaka 2010, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
kiliridhia ombi hilo na kupendekeza kukifanya Chuo cha Diplomasia kuwa
Chuo Kikuu cha Diplomasia na Stadi za Stratejia (College of Diplomacy and
Strategic Studies) chini ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Aidha, mchakato
wa Chuo kujisajili NACTE pia umefikia hatua za mwisho. Kukamilika kwa
mchakato huu kutakiwezesha Chuo kusajiliwa na NACTE na hivyo kuondoa
tatizo la muda mrefu la kutotambuliwa rasmi kwa kozi na shahada zake.
Muundo wa Chuo wa Awali
11.2.9 Kwa mujibu wa Katiba ya Chuo ya mwaka 1978, Chuo kina
ngazi kuu nne za utawala ambazo ni:
11.2.9.1 Baraza la Chuo: Hiki ni chombo cha juu cha sera na
utawala. Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza
wanateuliwa na Serikali za Tanzania na Msumbiji kama
ilivyoainishwa katika Katiba ya Chuo. Baraza lina
Kamati tatu ambazo ni Fedha, Mipango na Ukaguzi;
Taaluma; na Ajira na Nidhamu.
11.2.9.2 Mkurugenzi wa Chuo: Ndiye Mtendaji Mkuu wa
Chuo, ambaye huteuliwa na Mkuu wa Serikali wa
nchi mojawapo kwa kila kipindi kwa mujibu wa
Katiba ya Chuo. Mkurugenzi huwajibika moja kwa
moja kwa Baraza la Chuo.
62
11.2.9.3 Mkurugenzi wa Masomo na Programu: Ndiye
mkuu wa shughuli zote zinazohusiana na masuala ya
taaluma, ambaye huteuliwa na Baraza la Chuo.
Huwajibika moja kwa moja kwa Mkurugenzi wa
Chuo.
11.2.9.4 Afisa Utawala Mkuu: Ndiye mkuu wa kitengo cha
utawala cha Chuo, ambaye huteuliwa na Baraza la
Chuo. Huwajibika moja kwa moja kwa Mkurugenzi
wa Chuo.
Muundo wa sasa kwa mujibu wa masharti ya NACTE:
11.2.10 Mwaka 2009, Chuo kilianza mchakato wa mabadiliko ya
kimfumo na mitaala kulingana na vigezo vya NACTE. Kwa mujibu wa
masharti hayo muundo wa utawala, na ambao ndio unatumika sasa ni kama
ifuatavyo: Baraza la Chuo, Mkurugenzi wa Chuo, Naibu Mkurugenzi:
Taaluma, Utafiti na Ushauri na Naibu Mkurugenzi Mipango, Fedha na
Utawala. Mchakato wa kusajiliwa na NACTE utakapokamilika, nafasi hizo
zitatumia majina ya Mkuu wa Chuo (Principal) na Naibu Mkuu wa Chuo
(Deputy Principal), badala ya Mkurugenzi.
Majukumu na Malengo ya Chuo
11.2.11 Majukumu ya Chuo ni kutoa mafunzo na kufanya utafiti katika
masuala ya diplomasia, uhusiano wa kimataifa, stratejia, utatuzi na
usuluhishi wa migogoro na ujenzi wa amani. Lengo tarajiwa ni kukifanya
63
Chuo kuwa taasisi bingwa ya elimu ya juu na ushauri katika nyanja hizo.
Malengo ya jumla yamebainishwa katika Katiba ya Chuo Ibara ya 3 (a – g),
na ambayo ni kutoa mwamko katika nyanja za kijamii, uchumi na siasa kwa
kutoa mafunzo ya mahusiano ya kimataifa na mbinu za kidiplomasia;
kuendesha mipango ya mafunzo katika masomo ya mahusiano ya kimataifa
na diplomasia; kufanya utafiti juu ya matatizo na mahitaji ya fani hizo na
kutathmini matokeo ya mafunzo yaliyotolewa na mipango ya mafunzo kwa
ujumla; kutoa ushauri na huduma za kitaalamu kwa Serikali husika na taasisi
zake; kuandaa warsha au mikutano katika nyanja husika za Chuo;
kutayarisha machapisho na kutoa majarida yenye taarifa zinazohusiana na
kazi za Chuo.
Hali ya Uongozi na Utawala
11.2.12 Uongozi wa Chuo umepitia katika nyakati tofauti toka
kianzishwe. Jumla ya Wakurugenzi wanane wameshika nyadhifa hizo kama
inavyoonyeshwa katika Jedwali Na. VIII hapa chini:
Jedwali Na. VIII (Wakurugenzi)
Na. Jina la Mkurugenzi Muda
1. Bw. A. M. Hokororo 1978 - 1979
2. Bw. E. Seaton 1979
3. Balozi O. H. Tesha 1979 - 1984
4. Bw. A. M. Hokororo 1984 - 1989
5. Balozi N. Kiondo 1989 -1991
6. Dkt. I. S. Msabaha 1991 -1992
7. Prof. A. H. Omari 1994 - 2009
8. Balozi Dkt. M. O. Maundi 2010 hadi sasa
64
Sera na Sheria:
11.2.13 Kama ilivyoelezwa hapo awali, Chuo cha Diplomasia
kimeanzishwa rasmi kwa Mkataba baina ya Serikali mbili za Tanzania na
Msumbiji wa mwaka 1978, mjini Maputo, Msumbiji. Mwaka 1986, Chuo
kilijumuishwa katika Sheria ya Kinga na Upendeleo, Sheria Na. 5 ya mwaka
1986. Kimsingi, uendeshaji wa shughuli za Chuo unafuata Mkataba huo
ambao ulikuwa ndio msingi wa Katiba ya Chuo. Halikadhalika, Chuo
kinatekeleza majukumu yake kutokana na Sera ya Mambo ya Nje pamoja na
na Sera ya Elimu/Elimu ya Juu ya Tanzania na mabadiliko husika ya mara
kwa mara.
Sera na Sheria za ndani za Chuo
11.2.14 Baraza la Chuo ndicho chombo kikubwa na cha mwisho cha
kupitisha sera na sheria za uendeshaji Chuo. Katika kupitisha sera na sheria
hizo, Baraza huzingatia Sera na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania. Sera hizo za Chuo ni pamoja na sera ya utafiti, machapisho,
ushauri wa kitaalamu; sera ya walimu ya upimaji kazi na upandishwaji vyeo
na sera ya uendelezaji wafanyakazi mafunzo na ufadhili. Aidha, Chuo kina
Sheria Ndogo na Kanuni kadhaa zikiwemo: Kanuni za uendeshaji shughuli
za taaluma: Kanuni za mitihani; Kanuni za udahili na usajili wa wanafunzi;
Kanuni za uendeshaji wa jumuiya ya wanafunzi. Pia, Chuo kina Kanuni za
uendeshaji masuala ya utawala, Kanuni za utumishi, Kanuni za fedha;
Kanuni za matumizi na Kanuni za mavazi.
65
Mabadiliko na matukio muhimu pamoja na changamoto
zilizojitokeza
11.2.15 Katika mabadiliko ya kisiasa yaliyotokea nchini Tanzania
kutoka mfumo wa chama kimoja kwenda wa vyama vingi, Chuo, kama
zilivyo taasisi zote elimu za juu, hakikufungamana na chama chochote cha
siasa. Hivyo vuguvugu la kisiasa nchini kwa wakati wote halikuleta athari
yoyote ile katika utendaji wa Chuo.
11.2.16 Mabadiliko katika sera na hali ya ulinzi na usalama hapa nchini
na duniani kwa ujumla kumechangia katika marekebisho ya program za
mafunzo za Chuo. Chuo kimelazimika kufanya mapitio na uboreshaji wa
mitaala yake ili kujumuisha masuala muhimu ya nyanja za ulinzi na usalama
pamoja na stratejia. Pia, Chuo ni mwanachama wa Mtandao wa Utawala wa
Masuala ya Ulinzi na Usalama wa Kusini mwa Afrika.
11.2.17 Kupitia Mtandao wa Utawala wa Masuala ya Ulinzi na
Usalama, Wakufunzi wa Chuo na Wadau Wakuu wa masuala ya Ulinzi na
Usalama walipata mafunzo mbalimbali kukabiliana na mabadiliko katika
nyanja hizo. Kwa miaka kadhaa, Chuo kimekuwa kikiandaa mkutano wa
kila mwaka wa Amani na Usalama Kusini mwa Afrika. Mkutano huo
hufanywa kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi.
Shughuli zote hizi zimetoa mchango mkubwa katika kuwajengea uwezo
watendaji wetu na kuwafahamisha wadau na wananchi kwa ujumla juu ya
mabadiliko ya nadharia na vitendo yanayohusu masuala ya amani, ulinzi na
usalama duniani.
66
11.2.18 Kujitoa kwa Serikali ya Msumbiji katika kuchangia bajeti ya
Chuo na uendeshaji kumesababisha shughuli za uendeshaji wa chuo
kugharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tu.
11.2.19 Suala la teknolojia ya kisasa bado ni changamoto kwa Chuo,
hasa kwa kushindwa kuitumia kikamilifu katika shughuli zake za taaluma na
utawala.
Mafanikio
11.2.20 Chuo kinajivunia kuwa Chuo cha kipekee nchini Tanzania na
katika ukanda wa mashariki na kusini mwa Afrika kinachojumuisha taalum
na utaalamu wa vitendo.
11.2.21 Chuo kimeweza kutoa mafunzo mbalimbali katika nyanja za
diplomasia, mahusiano ya kitaifa,usuluhishi na utatuzi wa migogoro, ujenzi
wa amani, stratejia, ulinzi na usalama, na lugha za kigeni. Mafunzo hayo
yametolewa katika ngazi mbalimbali kwa kozi fupi na za muda mrefu.
Mafunzo hayo yametolewa kwa watumishi wa Wizara, taasisi na mashirika
ya Serikali, mashirika na makampuni binafsi, balozi na watu binafsi.
11.2.22 Chuo kimeongeza idadi ya program zake na udahili wa
wanafunzi kutoka 83 mwaka 2003 hadi 337 katika mwaka wa masomo
2010/2011. Aidha, kimetoa mafunzo kwa Watanzania zaidi ya 2,000 na
wengi waliopata mafunzo hayo wamenufaika kwa kuweza kuboresha
utendaji kazi wao.
67
11.2.23 Aidha, Chuo kimetoa mafunzo kwa maafisa zaidi ya 150 wasio
watanzania kutoka Afrika Kusini, Algeria, Angola, Botswana, Burundi,
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Kongo (DRC), Guinea, Kenya, Libya,
Malawi, Namibia, Palestina, Rwanda, Sudan, Zambia na Zimbabwe.
11.2.24 Chuo kimeweza kukarabati majengo yake. Jengo kuu
linalotumiwa kwa ofisi, hosteli na maktaba lilikarabatiwa mnamo mwaka
2004 na kuwa la kisasa. Pia, vyumba vya madarasa vimekarabatiwa sanjari
na iliyokuwa kantini na kuongeza madarasa, kujenga uzio na kuboresha
sehemu ya maegesho ya magari.
11.2.25 Chuo kimefanikiwa kuwaendeleza wafanyakazi wake kwa
kuwafadhili na kuwawezesha kupata mafunzo ya muda mrefu na mfupi
ndani na nje ya nchi. Jedwali Na. X hapa chini linaonyesha idadi ya
wafanyakazi walionufaika na ufadhili wa Chuo kuanzia mwaka 1987 hadi
sasa.
Jedwali Na. X (Wafanyakazi)
Idadi ya Wafanyakazi Programu ya Mafunzo
6 Udaktari wa Falsafa (Digrii ya Uzamivu)
7 Shahada ya Pili (Digrii ya Uzamili)
8 Shahada
6 Stashahada ya Uzamili
6 Stashahada
6 Cheti
21 Kozi fupi
Mahusiano na Taasisi Nyingine
11.2.26 Tangu kianzishwe, Chuo kimekuwa na mahusiano mazuri na
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ambayo ndiyo
Wizara Mama. Mara zote Wizara imekuwa mstari wa mbele kukisaidia
Chuo kwa njia mbalimbali katika kutatua matatizo yake yakiwemo ya
68
kiutawala na kifedha. Sambamba na hilo, Wizara imekisaidia Chuo kuingia
mikataba mbalimbali ya kitaaluma kama vile ushirikiano wa Taasisi ya
Mahusiano ya Nje na China na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
11.2.27 Chuo kimeendelea kuwa na mahusiano mazuri na Serikali na
Taasisi zake. Kimeweza kutoa mafunzo kwa wafanyakazi wa Wizara na
taasisi mbalimbali. Moja na mafunzo hayo ni Semina Elekezi ya Uongozi
yaliyotolewa kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka
2011 na Serikali ya Zanzibar ya mwaka 2006.
11.2.28 Aidha, Chuo kimekuwa na mahusiano mazuri na balozi
mbalimbali hapa nchini. Balozi hizo ni kutoka nchi za: Msumbiji, Angola,
Zambia, Marekani, Uingereza, Brazil, Ureno, Ujerumani, Libya, China,
Cuba, Afrika Kusini, Zimbabwe, Irani na Uganda. Aidha, kwa miaka mingi
Chuo kimeweza kuanzisha mahusiano na taasisi za kitaaluma za nchi za nje
zikiwemo: Chuo Kikuu cha Newcastle cha Australia, Chuo Kikuu cha Iran,
na Taasisi ya Mahusiano ya Kimataifa ya China.
11.2.29 Mchango wa chuo umekuwa mkubwa sana katika ujenzi wa
Taifa letu. Mchango huo umekuwa ni pamoja na kuifahamisha na kuishauri
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa katika masuala ya
utekelezaji wa shughuli zake muhimu. Chuo pia kimekuwa kikijikita katika
utatuzi wa migogoro, kutoa mafunzo, tafiti na ushauri wa kitaalamu katika
masuala ya itifaki, diplomasia ya uchumi, stratejia na menejimenti ya
mahusiano ya nje.
69
12.3 Taasisi ya APRM Tanzania
12.3.1 APRM ni kifupi cha “African Peer Review Mechanism” ambao
ni Mpango wa Nchi za Umoja wa Afrika uliobuniwa na viongozi wa Umoja
huo mwanzoni mwa miaka ya 2000 ili kujitathmini zenyewe katika masuala
ya utawala bora. Katika mpango huo, nchi husika hujitathmini yenyewe
kwanza na kutoa ripoti ya ndani na kisha hufanyiwa tathmini na nchi
nyingine za kiafrika zilizojiunga katika mpango huo.
12.3.2 Tanzania ni moja kati ya nchi 30 zinazoshiriki katika mpango
huo na ilijiunga tarehe 26 Mei, 2004 kwa Azimio la Bunge la kuridhia
Mkataba wa Umoja wa Afrika wa uanzishwaji wa mpango huo. Uridhiaji
huo ulifanyika tarehe 1 Februari 2005. Mnamo mwaka 2006 vyombo
muhimu vya usimamizi wa mpango huo vilianzishwa.
Muundo wa APRM-Tanzania
12.3.3 Muundo wa mpango huu ni kama ifuatavyo:
12.3.3.1 Wizara Mama:
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa
ndiyo Wizara Mama katika Tanzania. Majukumu yake ni
kurahisisha mawasiliano kati ya vyombo
vinavyoshughulikia APRM ndani ya nchi na pia kati ya
nchi na Umoja wa Afrika. Aidha, Wizara Mama
hushirikiana na APRM katika matayarisho ya bajeti ya
shughuli zake na kutafuta misaada ya fedha kutoka kwa
washirika wa maendeleo.
70
12.3.3.2 Baraza la Taifa la Usimamizi wa APRM
Hiki ni chombo kinachosimamia utekelezaji wa
majukumu ya APRM katika Tanzania na ambacho ni
chombo huru kisichoingiliwa kisiasa. Baraza hilo lina
wajumbe 20 kutoka sekta mbalimbali muhimu, zikiwepo
vyama vya siasa, madhehebu ya kidini, asasi za kijamii,
vyombo vya habari na wajumbe wanne wanaoiwakilisha
Serikali. Baraza hili, lilizinduliwa rasmi na Mhe. Jakaya
M. Kikwete, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa
Tanzania tarehe 11 Septemba 2009.
12.3.3.3 Sekretarieti ya APRM ya Taifa
Sekretarieti ya APRM Tanzania inaongozwa na Katibu
Mtendaji ambaye anasaidiwa na Waratibu watatu. Aidha,
kuna Afisa Mawasiliano na Meneja wa Matukio ambao
hutoa huduma za mawasiliano na kufanikisha matukio
mbalimbali. Katibu Mtendaji wa sasa aliteuliwa mwezi
Januari 2010 baada ya Katibu Mtendaji aliyetangulia
kumaliza muda wake. Kazi za Sekretarieti ya APRM ya
Taifa ni pamoja na kuratibu mchakato wa APRM ndani
ya nchi, kutoa huduma za kitaalam na kiutawala kwa
Baraza la Taifa la Usimamizi wa APRM, kuendesha
semina za uelimishaji kuhusu mchakato wa APRM katika
ngazi za kitaifa, mikoa na vijiji na kuratibu kazi za taasisi
za kitaalam zinazofanya tathmini ya utawala bora.
71
Majukumu na Malengo toka ianzishwe hadi sasa
12.3.4 Majukumu makuu ya APRM Tanzania ni kusimamia tathmini
ya utawala bora katika Tanzania na hatimaye kuratibu utekelezaji na
kuondoa mapungufu ya utawala bora yatakayokuwa yamebainika katika
Ripoti ya Tathmini ya Utawala Bora.
Hali ya Uongozi na Utawala
12.3.5 Tangu kuanzishwa kwake, Baraza la Taifa la Usimamizi wa
APRM Tanzania limeendelea kusimamia mchakato na Sekretariati ya
APRM Tanzania kwa ufanisi mkubwa. Baraza huwa na vikao vinne kwa
mwaka. Baraza pia limeunda kamati mbalimbali zinazosimamia maswala ya
Fedha na Utawala, Mipango pamoja na Mawasiliano na wadau. Hadi sasa
hapajawa na mabadiliko katika uwakilishi ndani ya Baraza.
12.3.6 Uongozi wa APRM na Baraza la Taifa la Usimamizi
zinaoneshwa katika Jedwali Na. XI hapa chini:
Jedwali Na. XI (Uongozi wa Baraza)
S/N Jina Taasisi
Anayowakilisha
Mwaka Alioanza Mwaka wa Kumaliza
Sekretariati ya APRM ya Taifa
1. Prof. Daudi Mukangara Katibu Mtendaji
(APRM)
2007 Machi 2009
2. Bi. Rehema Twalib Katibu Mtendaji
(APRM)
2009 Hadi sasa
Wajumbe wa Baraza la Taifa la Usimamizi wa APRM Tanzania
1. Prof. Hasa Mlawa Chuo Kikuu cha DSM Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
2. Bi. Oliva Kinabo
(Makamu Mwenyekiti)
Baraza la Maaskofu
Tanzania (TEC)
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
3. Bi. Tecla W. Shangali Tume ya utumishi wa
Umma
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
72
4. Prof. Ruth Meena Mtandao wa Jinsia
Tanzania (TGNP)
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
5. Bw. Pelemon Rujwahula Chama cha Walemavu
Tanzania (CHAWATA)
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
6. Bw. Peter Masika Muungano wa Vijana
Tanzania (TAYOA)
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
7. Prof. Ibrahim Shao Chuo Kikuu cha DSM Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
8. Bw. Said Muhammed Wizara ya Mambo ya
Katiba na Utawala Bora,
Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
9. Bw. Samson Chemponda Baraza la Taifa la
Biashara (TNBC)
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
10. Bw. Willigis Mbogoro Muungano wa Vyama
vya Ushirika (TFC)
Barua yake haitaji ukomo
11. Bw. Nestory Masswe Muungano wa Vyama
Visivyo vya Kiserikali
(TANGO)
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
12. Bw. Wilson Mallya Chama cha Wakulima
Tanzania (TFA)
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
13. Dr. Salim S. Nasser Sekta Binafsi, Zanziar Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
14. Mhe. John Magalle
Shibuda
Bunge la Tanzania
(Upinzani)
Februari 2011 2015
15. Ipo wazi Tanzania Chamber of
Commerce, Industry and
Agriculture (TCCIA)
Novemba 2006 Mwakilishi alikuwa
Bw. Elvis Musiba
(Amefariki)
16. Bi Rosemary Jairo Tume ya Haki za
Binadamu na Utawala
Bora (CHRAGG)
Novemba 2006 Barua yake haitaji ukomo
17. Sheikh Suleiman Lolila Baraza la Waislam
Tanzania (BAKWATA)
2010 Barua yake haitaji ukomo
18. Bw. Anthony Ngaiza Baraza la Habari (MCT) Barua yake haitaji ukomo
19. Bw. Mathew Mhina
Mwaimu
Wizara ya Sheria na
Mambo ya Katiba
Mei 2007 Barua yake haitaji ukomo
20. Bi. Martha Jachi Umbulla Bunge la Tanzania
(Chama Tawala)
Mei 2011 2015
Chanzo: Sekretarieti ya APRM
Sera na Sheria zinazoongoza taasisi hiyo hadi sasa
12.3.7 Kama ilivyoelezwa hapo juu, APRM iliundwa baada ya Bunge
kuridhia Mkataba wa Umoja wa Afrika wa uanzishwaji wa Taasisi hiyo na
inaongozwa kwa kuzingatia sheria za nchi, kanuni na taratibu mbalimbali
zinazopitishwa na Baraza la Usimamizi wa APRM Tanzania. Mpaka sasa
APRM inazo Kanuni za Fedha (Financial Regulations) na Muundo wa
73
Utumishi (Staff Regulations) ambazo zinatumika kusimamia mapato na
matumizi ya fedha pamoja na rasilimali watu.
Mafanikio yaliyopatikana hadi sasa
12.3.8 Kufahamika kwa mchakato wa APRM kwa wadau wengi:
APRM Tanzania imeendesha semina elimishi kwa wadau wapatao 5,000
wakiwemo Waheshimiwa Wabunge, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi,
Makatibu Wakuu, Makatibu Tawala, Jamii ya Wasomi, Viongozi Wanawake,
Viongozi wa Vyama vya Siasa na Majaji.
12.3.9 Kuandaa Ripoti ya Ndani ya Utawala Bora (Country Self
Assessment Report): APRM Tanzania iliratibu tathmini ya utawala bora
nchini na kufanikiwa kukamilisha Ripoti ya Tathmini ya Ndani ambayo
iliwasilishwa Sekretarieti ya APRM ya Umoja wa Afrika tarehe 14 mwezi
Julai 2009. Ripoti hiyo imebaini mambo mazuri yaliyofanywa na Serikali
katika miaka mitano iliyopita ambayo nchi nyingine zinaweza kuyaiga.
Aidha, ripoti imebaini mapungufu ya utawala bora nchini ambayo
yanatakiwa kufanyiwa kazi. Rasimu ya Mpango Kazi wa kuyaondoa
mapungufu hayo pia iliandaliwa.
12.3.10 Uzoefu: Mchakato wa APRM umeziwezesha taasisi za utafiti
na wataalam wa ndani ya nchi kujiongezea uzoefu wa kufanya tathmini juu
ya utawala bora katika nchi yao na hivyo kuongeza hazina ya utaalam wa
tathmini ya aina hii katika nchi yetu.
74
Changamoto
12.3.11 Kutokana na mahitaji makubwa ya fedha katika kuendesha
semina za kuelimisha umma na kwa uhamasishaji wa ana kwa ana, vyombo
vya habari ikiwemo redio, TV na magazeti ndivyo vilitumika zaidi.
12.3.12 Kuchelewa kuja kwa ujumbe maalum kutoka Sekretarieti ya
Umoja wa Afrika kwa ajili ya kufanya tathmini ya nje hapa nchini.
Matarajio katika miaka 50 ijayo:
12.3.13 Kuimarisha APRM inayojitegemea.
12.3.14 Kuimarisha zaidi utawala bora na hivyo kudumisha utulivu wa
kisiasa na kuwezesha maendeleo ya haraka zaidi ya kiuchumi na
kijamii.
WIZARA YA MAMBO YA NJE NA
USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
30 JUNI, 2011

4 comments:

  1. Repeat this timetable just about every single 15th times.
    Pure cotton silk that is soft best are almost always well priced
    as well, so that you could apparel various things to get once the!
    The organization with which to find yourself utilized with the
    outback, Ugg boot have taken compromised according to
    attack. Additional, not lumpy and bumpy skin therapies could actually work as much concern intensity.
    If you don't have Adobe Acrobat installed in your hard drive, you will find there's
    url to downloading Adobe Acrobat cost free.

    Look at my web page ... coffeemakersnow.com

    ReplyDelete
  2. You have to starting confirm the KitchenAid food processor or blender
    elements the particular street bike become faulty.

    In contrast, while you are headed for a comprehend, the outgoings tend to
    be worth purchasing. First, simply Blender or food processor you are able to pose?

    Is Fantastic superb decor this important blender has a A variety of.
    A couple of Hp engine's motor complete with heightens in order to really 40,Five hundred, RPM causing it to useful for dining establishments in addition profitable assist.

    Have a look at my site good quality blender australia

    ReplyDelete
  3. Cleanup an Acme Juice extractor is rarely complexed.
    Years is going to be years into the future additionally the providers are quite certain of her services or products to
    supply a here interminable manufacturer's warranty. Such juice machine is suffering from a nominal effect, for that reason it befits correctly without taking enhance much room from the; but never let weight twit your entire family onto thought it is not useful. The foregoing machine really cost-effective.

    Have a look at my blog post - high rpm blenders

    ReplyDelete
  4. That has a dimension at 42x 30x 26 cm, it is certainly
    large enough when you need to contributes to methods with
    the food prep. What kind of many advantages you need to and desire have always
    been that which will need to have your family deciding to, earning you money are
    plenty of to select thanks to frequently. Logic says
    matter to get a vita mixer package is the
    decanter or wineglass. Additional, specific pigment using the green hued with all the vegetables or flowers is
    also chlorophyll.

    Feel free to surf to my weblog ... best blenders

    ReplyDelete